TANGAZA NASI LEO 0712709630,0756631636 BARUA PEPE gmkojera@gmail.com

Tuesday 20 March 2012

Hadija asimulia mwanaye alivyotendewa ukatili na vijana wa mtaani



Na Grace Mkojera
Ukatili dhidi ya wanawake ni ukiukwaji ulionea wa haki za binadamu, ni janga kubwa katika jamii na kikwazo cha kufikia usawa, maendeleo, usalama na amani. Wakati wengine wakifurahia amani kuna wengine wanalia kwa kutendewa ukatili.
Inakadiriwa kuwa mmoja kati ya wanawake watatu duniani atakumbana na aina fulani za ukatili wa kijinsia katika maisha yake.
Takwimu za mwaka 2010 za TDH zinaonyesha kuwa robo tatu ya wanawake wa kitanzania wenye umri wa kati ya miaka 15 hadi 49 wameshafanyiwa vitendo vya ukatili kwa mwaka.
Utafiti wa mwaka 2009 unaonyesha kuwa watoto wa Tanzania 6 kati ya 10 wasichana na wavulana wana uzoefu wa ukatili kutoka kwa walimu hao.
Aidha, siku 16 za kupinga ukatili wa kijinsia zimekuwa zikiadhimishwa na watu binafsi pamoja na makundi duniani kote wanaotumia mtizamo wa haki za binadamu ili kutoa mwito wa kutokomeza aina zote za ukatili dhidi ya wanawake kwa kuelimisha jamii na kuishinikiza serikali kutekeleza maazimio ya kisheria yaliyofikiwa kitaifa na kimataifa.
Katika maadhimisho yaliyoandaliwa na Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP) kwa kushirikiana na washiriki wa semina za jinsia na maendeleo (GDSS), kuna baadhi ya wadau mbalimbali ambao walitoa visa mkasa vinavyowanyima usingizi mtaani.
Mmoja wa washiriki kwenye maadhimisho hayo ni Hadija Rashid ambaye ni mkazi wa Kiburugwa jijini Dar es Salaam, anaeleza machungu ambayo yamekuwa yakimkosesha raha na familia yake.
Ni mama wa familia ya watoto 7 ikiwa ni mchanganyiko wa watoto wa kike na wa kiume. Katika watoto wake wa kike wawili mmoja anasoma kidato cha pili anayeitwa Amina Mohamed na mwingine anaitwa Rahma Mohamed ambaye hasomi hawana raha ya maisha kutokana na vita na majaribu anayokutana nayo.
Mama huyo anaelezea kuwa watoto wake hao pindi ambapo wako mtaani kuna kikundi cha vijana katika mtaa wanaoishi ambao wamekuwa wakiwasumbua na kuwatongoza.
Watoto hao wamekuwa wakiwakatilia vijana hao hasa ikizingatia kwamba mmoja ndio huyo anasoma bado ni mwanafunzi na mwingine ameamua kujiheshimu hivyo wote waliwakatalia.
Katika kundi hilo la vijana zaidi ya 10 ambao hupenda kukaa kijiweni katika jumba moja bovu, wamekuwa wakitoa vitisho kwa wasichana hao. Kumbe kila mmoja anapowajaribu wasichana hao na kukataliwa huambizana hivyo hupanga mkakati wa kuwakomesha.
Anaelezea kuwa watoto wake hao pindi wanapoenda kuchota maji hukutana na kundi hilo wakiwa wanawasubiri na kuwatukana huku wengine wakiwaeleza wazi wazi kuwa lazima wawabake waone wanachoringia ni kitu gani.
Maneno makali ambayo yamekuwa yakitolewa na vijana hao yamekuwa yakiwapa hofu ya maisha. Ndipo mama huyo alipoamua kwenda kutoa taarifa katika kituo cha Polisi Kiburugwa na kupewa RB huku wakiahidiwa kuwa watakuja kuwakamata vijana hao.
Baada ya wiki moja Polisi hawakutokea kuwakamata vijana hao bali waliendelea kukaa kimya. Ikawa kila wale watoto wanapotumwa kwenye maji ama kwenda kutafuta kuni inabidi waende wawili wawili kwasababu tayari walishatishiwa kubakwa.
Anasema kuwa ili watoto wake wasikumbwe na vitisho hivyo pia aliulizia mahali wanapoishi vijana wale ili kuzungumza na wazazi wao kuhusiana na vitisho wanavyotoa na kuahidiwa na wazazi wao kuwa watazungumza na vijana wao.
Lakini anasema taarifa ile haikusaidia bado wale vijana waliendelea na vitisho mara kwa mara. Kila wanapowaona wale wasichana wakiwa peke yao hutokea ghafla na kuwazingira na kuwavutia pembeni bila kuogopa kwamba kuna watu wanaopita watawaona.
Anasema kwa bahati siku ya kwanza ambapo kundi hilo la vijana liliwazingira wasichana hao ili wawabake kulikuwa na mzee mmoja wa kilokole ambaye alikuwa akipita na kuona lile tukio ndipo kuwaokoa wasichana hao hivyo walinusurika.
Wiki ya pili baada ya mama huyo kuona hakuna mafanikio anasema akaenda tena kituo cha Polisi kutoa taarifa dhidi ya tukio hilo lakini hakuna hatua yoyote iliyochukuliwa.
“Ndipo nikaenda tena kwa wazazi wa wale vijana kwa mara nyingine na kupewa RB, lakini bado hawakukamatwa,”anasema.
Anasema siku nyingine alimtuma tena mtoto yake  ambaye hasomi aende kununua kuni, ilikuwa ni majira ya saa tisa jioni huku mdogo wake ambaye ni mdogo mwenye umri wa miaka 9 akimsindikiza.
Wakati wanarudi mara wakatokea vijana 2 wakawazingira na kumlazimisha Yule dada atupe kuni chini na kumkamata. Yule mtoto mdogo alifanikiwa kukimbia. Hawakujali bali waliendelea na Yule mkubwa wakamfunga kamba miguuni na mikononi  huku kijana mwingine akisema kuwa “tumvunje mbavu,”
Anasema wakati kijana mmoja akisema wamvunje mbavu kwasababu yule binti alikuwa ni mbishi anajaribu kujinasua ili apate kuokoka, Yule kijana mwingine akasema “tumpige na jiwe kichwani ili apoteze fahamu ili kuwa rahisi kumaliza kazi  ya kubaka,”
Anazidi kusimulia huku machozi yakimtoka kuwa wakati Yule mmoja akienda kutafuta jiwe, Yule kijana mwingine tayari alikuwa na wembe ameuweka kiganjani hivyo aliutumbukiza kwenye vidole na kumpiga nao Yule msichana usoni.
Hata hivyo, kabla hawajafikia zoezi lao la kumpiga jiwe kichwani ili wamalize kazi yao, kwasababu Yule mtoto mdogo alikimbilia nyumbani kutoa taarifa kwa wazazi, waliwahi kuja na kumwokoa.
“Sehemu alipokamatiwa binti yangu sio mbali sana na nyumbani, tuliweza kuwahi mapema na kumwokoa,”anasema Bibi Hadija.
Anasema kuwa wale vijana walipowaona walikimbia, na ndipo mama huyo kukimbilia tena Polisi Kizuiani baada ya kuona Kiburugwa hawakuwapa msaada wowote.
Kwa bahati nzuri mkuu wa Polisi kiuziani kwa kushirikiana na wenzake waliona jambo hilo sio la kuvumilia, walienda kuwatafuta vijana hao na kufanikiwa kuwakamata.
Walifanikiwa kufungua kesi katika mahakama ya kizuiani, hata hivyo vijana hao tayari walishaachiwa kwa dhamana wako mtaani, ila kesi bado inaendelea kusikilizwa.
Pamoja na harakati zote hizo za kuwaokoa watoto wake bado anakabiliwa na changamoto kubwa, jamii inayomzunguka haijashirikiana naye katika kupambana na vijana hao hatari.
Anaeleza imekuwa ni kawaida kwa vijana hao kuwabaka wasichana na kuwapa mimba. Wasichana wengi wanaoishi katika mtaa wake wamepata mimba na wala hawana msaada wowote.
Na bado wanaendelea na vitendo vya kikatili na wanakaa kimya badala ya kuweka umoja wao ili vijana hao wachukuliwe hatua kali za kisheria. Bado baadhi ya wazazi wa vijana hao wengine wamekuwa wakimlaumu Hadija kwa kuwafungulia wanawe kesi na wengine walimvamia na kumpiga hadi kupoteza fahamu.
Ukatili huo hauhitajiki kufumbiwa macho, jukumu ya kupinga vitendo hivyo liingiliwe na jamii ili kunusuru maisha ya watoto wa kike. Kuendelea kunyamaza bila kusema chochote wala kuchukua hatua ukatili utaendelea kuongezeka.
Mwisho.

No comments:

Post a Comment