TANGAZA NASI LEO 0712709630,0756631636 BARUA PEPE gmkojera@gmail.com

Tuesday 20 March 2012

Simu zinaposaidia kukuza wateja


Kazaura katikati akiwa katika maonyesho ya bidhaa zake na wasaidizi wake


















Unajua kuwa simu husaidia kukuza biashara yako?

Wilson Kazaura ni mjasiriamali wa bidhaa mbalimbali ambaye amekuwa akiuza bidhaa mbalimbali za nafaka ambazo hulimwa mkoani Kagera zikiwemo maharage, njugu mawe, nyanya chungu ndogo ndogo, mpala,  mashasha, senene na Samaki aina ya pina ya mboju.
Bidhaa nyingine ni pamoja na vikapu ambavyo hutumika kutolea mahari kwa wahaya, kata ya kubebea kikapu hicho, vibuyu ambavyo hutumika kunywea pombe za asili, kahawa, pilipili na vitu vingine
Kazaura anaeleza kuwa kabla ya kuanza kuuza bidhaa hizo, mwaka 2004 alianza biashara ya samaki ambapo alikuwa akisafiri Mwanza, Musoma na Kagera na kununua bidhaa hiyo kwa wachuuzi wadogo na baadaye kurudi Dar es Salaam na kuanza kutembeza nyumba kwa nyumba.
Wakati anafanya hivyo alikuwa akiendelea kutengeneza mtandao kila mahali anapopitisha bidhaa hiyo ya samaki. Anachukua namba za simu za wateja wake na kuzihifadhi ili anapokuja na bidhaa mpya awajulishe wateja na hivyo kuwafikishia kiurahisi.
Anasema “kule ambako nilikuwa naenda kuchukua samaki nilikuwa naendelea kutengeneza mtandao na wale wachuuzi hivyo walianza kuniamini na baadaye nikaona sasa niagize kwa wale wachuuzi waniletee kuliko niwafuate kule,”
Kwa vile tayari alikuwa na mtandao mkubwa biashara hiyo ya samaki ilianza kumwendea vizuri na hivyo kukuza mtaji wake kwani kwa kadri siku zilivyokuwa zinakwenda nay eye ndivyo alivyokuwa akizidi kutengeneza mtandao wa kibiashara ambapo alipata wateja wengine wakubwa katika mahoteli mbalimbali jijini Dar es Salaam waliokuwa wakimwagiza awapelekee samaki.
“Namshukuru Mungu kutokana na juhudi zangu watu waliniamini nikawa napata oda nyingi ambapo nilikuwa naleta samaki wengi na nilikuwa nafanikiwa kumaliza ndani ya siku moja, kwani nilikuwa nikipata samaki nawajulisha wateja wangu na hivyo kuniagiza niwapelekee,”anasema.
Baada ya mwaka mmoja, Kazaura alipata wazo la kufungua duka ili aweze kuendeleza biashara sio tu upande wa samaki bali pia kuuza bidhaa nyingine. Lakini mawazo yalikuwa tofauti na wajasiriamali wengine kwani yeye aliona ni bora auze bidhaa zinazotoka mkoani Kagera ambako ndiko alikozaliwa ili kuwaunga mkono wakulima wa mkoa huo.
Anasema  duka lake lipo Sinza na wateja wake wakubwa ni wahaya wenzake na wamekuwa wakitoka sehemu mbalimbali hadi eneo hilo ili tu kufuata bidhaa za kwao ambazo zimeonekana kuwa kivutio kikubwa.
Utaratibu aliojiwekea katika duka lake ni wa ubunifu wa aina yake na bado maduka mengi katika sehemu mbalimbali bado hawajaugundua. Kwanza ukifika katika duka lake unakaribishwa kwa ukarimu na mara unaponunua bidhaa kuna kitabu kwa ajili ya wateja ambapo unaandika jina lako na kuweka namba za simu ili kuwa rahisi anapoleta bidhaa mpya kujulishwa.
Anasema simu ambazo huachwa na wateja wake huhifadhiwa kwa uaminifu, ambapo mara tu bidhaa zinapoingia kutoka Bukoba kila mteja aliyeacha namba yake ya simu anatumiwa ujumbe mfupi wa kumjulisha kwamba tayari mzigo umeingia hivyo wanakaribishwa kutembelea duka hilo na kuchagua kile wanachokitaka kulingana na bei anayoweza mteja.
Na anachojivunia ni kuungwa mkono na wahaya wenzake kwa asilimia kubwa kwa vile zile bidhaa nyingi hufahamika kwa Wahaya. Na wanapoenda katika duka lake wanakuwa na uhakika wa kujikumbushia utamaduni wa vyakula vyao walivyivisahau.
Wateja wake sio tu kwamba wapo Sinza peke yake, bali wanaishi Mbagala, Kawe, Kimara, Bunju, Kigamboni na karibu sehemu zote za Dar es Salaam. Wamekuwa wakisafiri kutoka maeneo wanayoishi hadi Sinza bila kujali kwamba kuna umbali mkubwa wa safari yenyewe.
Lakini Kazaura anasema wateja wake wamekuwa wakilalamikia ugumu wa usafiri wakati mwingine, hivyo ili kuwaridhisha anajipanga ili kuhakikisha anafungua matawi manne ambako wateja ndiko wanakotokea kwa wingi ili kuwarahisishia wateja wake.
“Baada ya miaka miwili ndio nitaangalia uwezekano wa kufungua matawi manne kwa ajili ya kuwafikishia wateja wangu huduma karibu ili wasipate shida kwasababu kuna wengine wanalalamikia ugumu wa usafiri,”anaeleza Kazaura.
Kazaura anasema wakati anaanza biashara alikuwa akijikuta kwenye wakati mgumu hasa pale ambapo mtaji ulikuwa unakata kutokana na bidhaa nyingine kuoza. Lakini hakukata tamaa zaidi aliona ni bora akope aendeleze biashara yake na ndipo kufanya hivyo na hatimaye leo anajivunia kwa mafanikio anayoyapata.
Kitu anaona ni kikwazo kikubwa katika biashara yake ni kukatika kwa umeme kila wakati. Anasema kitendo hichi kimesababisha hasa  katika bidhaa zake hasa zile ambazo hutegemea friji zimekuwa zikioza na hivyo kusababisha hasara.
Anachopendekeza ni Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) kufanya jitihada za kupunguza tatizo la umeme kama ambavyo wameahidi wananchi. Anasema tatizo hilo iwapo litapungua litawasaidia wafanyabiashara wengi kuokoa mali zao.
 Mjasiriamali huyo anasema kupitia biashara hiyo amefanikiwa kujenga nyumba ya kisasa, kuwapeleka watoto wake katika shule nzuri pamoja na kuendelea kukuza mtandao wa biashara.
Anasema hajawahi kushiriki katika maonyesho yoyote ya kibiashara, kufika kwake katika maonyesho ya Wahaya ni fursa anayojivunia. Anaamini kuwa huo ni mwanzo kwa vile tayari ameshafunguliwa njia anajipanga ili aweze kushiriki katika maonyesho makubwa ya bidhaa kama vile Sabasaba ili azidi kutangaza biashara yake.
Anasema siri nyingine iliyomwezesha kujenga mtandao ni kwamba sio tu huwajulisha wateja wake kuhusiana na bidhaa mpya, bali pia msimu wa sikukuu huwatumia wateja wake wote ujumbe mfupi wa maneno kwenye namba za simu za wateja  kuwatakia heri ya sikukuu. Kwa njia hiyo pia mteja anajivunia na kuvutiwa zaidi.
Vijana wengi huogopa kuthubutu na wengine hawana ubunifu wa kuwavutia wateja ili kesho aweze kurudi tena. Matokeo yake wanapoanza biashara huishia njiani na wengine wanakula mtaji na wengine hukata tamaa pale wanapoona wanapata hasara fulani.
Kazaura anawaeleza vijana kutokata tamaa, jambo la muhimu ni kuthubutu. Anasema kuna wengine wanaogopa kupitisha bidhaa mtaani kwasababu tu ni msomi hivyo anaogopa kuchekwa, wengi wanataka kufanya kazi za ofisini.
“Unapotaka kufanikiwa usiogope wala kuchagua kazi, jenga uaminifu, jitoe muhanga, usitegemee kazi za ofisini ili uajiriwe, kufanya kazi kwa bidii na kwa uaminifu ni njia pekee itakayokuwezesha kufanikiwa kibiashara,”anasema Kazaura.
Vijana ambao huogopa biashara wanaweza kujifunza kupitia kwa mjasiriamali huyu, amepitia vikwazo vingi lakini hakukata tamaa na leo ameweza kutimiza ndoto yake.
Mwisho.

No comments:

Post a Comment