Sekretarieti
ya Ajira katika Utumishi wa Umma ni chombo kilichoundwa kwa mujibu wa Sheria ya
Utumishi wa Umma Na. 8 ya mwaka 2002 kama
ilivyorekebishwa na Sheria Na. 18 ya mwaka 2007 kifungu 29 (1).
Ni
vyema tufahamu kuwa chimbuko la Sekretarieti ya Ajira katika Utumishi wa Umma
limetokana na maboresho yanayoendelea katika Utumishi wa Umma nchini. Ambapo miongoni mwa maboresho hayo ni pamoja
na marekebisho ya Sera ya Menejimenti na Ajira katika Utumishi wa Umma ya mwaka
1998 toleo Na. 2 la mwaka 2008 ambapo katika Vifungu Na. 4.6 na 6.6. vya Sera hiyo ambavyo vimetamka
kuwepo kwa chombo maalum cha kushughulikia mchakato wa masuala ya ajira katika
Utumishi wa Umma.
Kwa
mujibu wa Sheria, Sekretarieti ya Ajira katika Utumishi wa Umma ndio chombo
pekee chenye wajibu wa kutekeleza majukumu
yafuatayo:-
i)
Kutafuta wataalam wenye ujuzi maalum na kuandaa
mfumo wa kuhifadhi taarifa za wataalam.
ii) Kutangaza
nafasi wazi za kazi zinazojitokeza katika Utumishi wa Umma.
iii) Kuhusisha
wataalam maalum ili kushirikiana nao kwa ajili ya kufanya usaili kulingana na
mahitaji.
iv) Kuwashauri
waajiri kuhusu masuala mbalimbali yanayohusiana na mchakato wa ajira.
v)
Kuandaa orodha ya wahitimu wa Vyuo na wataalam
weledi kwa madhumuni ya kurahisisha rejea za ujazaji wa nafasi za ajira katika
Utumishi wa Umma.
Aidha,
kwa mujibu wa Sera hiyo, kuwepo kwa chombo hiki kutaziwezesha Mamlaka za Ajira
nchini (zikiwemo zile za Serikali Kuu na Mamlaka za Serikali za Mitaa) kubaki
na majukumu yake ya msingi (Core functions) ambayo yameainishwa katika uundaji
wa Mamlaka hizo ili kuongeza ufanisi.
Kutokana
na maelezo hayo hapo juu ni vyema
wananchi wote wakafahamu kuwa ni kosa kwa mtu au taasisi yeyote ile kuchukua Matangazo
ya Sekretarieti ya Ajira na kuyafanyia marekebisho au kuandaa matangazo
mbalimbali yanayohusiana na mchakato wa ajira katika Utumishi wa Umma kwa lengo
la kupotosha umma ilihali wakijua wazi kuwa taarifa hizo wanazozichapisha au
wanazoziandika katika mitandao ya kijamii hazijatolewa na Sekretarieti ya Ajira
katika Utumishi wa Umma.
Tumefikia
hatua ya kusema haya kutokana na baadhi ya taarifa zinazohusu mchakato wa ajira
hususani uwepo wa nafasi za kazi zilizopo katika baadhi ya mitandao ya kijamii
ikionyesha kuwa Katibu wa Sekretarieti ya Ajira ametoa matangazo hayo.
Moja
ya tangazo hilo la kughushi na lenye nia
ya kupotosha umma ni lile lililoko katika anwani hii www.eastafricajobscareer.com lenye
kichwa cha habari kinachosomeka “Tangazo la Kazi Utumishi Tanzania June 2013” ambalo linaonyesha “Mwisho wa kupokea barua za maombi ni tarehe 8 Juni, 2013”.
Katibu
anapenda kuwasisitizia wadau wote wa Sekretarieti ya Ajira wanaotafuta kazi
pindi wanapoona matangazo katika Vyombo mbalimbali vya Habari wajiridhishe kwa
kuthibitisha taarifa hizo kama ni za kweli kwa kutembelea tovuti ya
Sekretarieti ya Ajira ambayo ni www.ajira.go.tz kwa taarifa
sahihi zihusianazo na ajira katika Utumishi wa Umma.
Sekretarieti
ya ajira haiwajibiki na wala haitawajibika kwa Matangazo ama taarifa zozote zinazohusiana
na mchakato wa ajira katika Utumishi wa
Umma ambazo haijazitoa rasmi.
Imetolewa
18 Machi, 2013 na
Katibu,
Ofisi
ya Rais,
Sekretarieti
ya Ajira katika Utumishi wa Umma
Maktaba
Kuu ya Taifa/Barabara ya Bibi Titi Mohammedi
S. L.
P 63100, Dar Es Salaam.
Simu;
+255 22 2153517
Nukushi;
+255 22 2153518
Barua pepe: katibu@ajira.go.tz
Tovuti; www.ajira.go.tz
Aidha, kwa maelezo
zaidi; wasiliana na Kitengo cha Mawasiliano
Serikalini kwa Barua
pepe; gcu@ajira.go.tz au
Simu;
255-687624975
No comments:
Post a Comment