Mwimbaji nguli wa muziki wa tarabu nchini Tanzania
Fatma binti Baraka, maarufu kama Bi Kidude amefariki Jumatano kisiwani
Zanzibar akiwa na umri wa zaidi ya miaka 100.
Bi Kidude amekuwa katika fani ya muziki wa taarab ya kiasili pamoja na ngoma za unyago kwa zaidi ya robo tatu ya umri wake.
Bi. Kidude |
Wengi, hasa vijana wa kizazi kipya wanamfahamu Bi. Kidude kwa uwezo wake mkubwa wa kuimba taarabu kwa kuchanganya lugha ya kiswahili na ile ya kiarabu. Nyimbo zake za kiarabu mara nyingi zimekuwa na ladha kama ile ya aliyekuwa mwimbaji gwiji wa Misri Ummu Kulthumu.
Sio uimbaji tu uliomfikisha Bi. Kidude alipofika, bali uwezo wake pia wa kutunga mashairi, kutumia ala za mziki kama vile kupiga ngoma na hata ngoma za unyago, vyote hivi vilimuweka Bi. Kidude katika nafasi tofauti katika jamii.
Alikuwa na tabia ya kumwita kila mtu 'mwanangu,' ingawa yeye mwenyewe hakubahatika kupata mtoto. Katika mahojiano aliyofanyiwa na vyombo mbali mbali vya habari, mwenyewe alisikika akisema, ingawa alikuwa na hamu ya kupata mtoto, lakini Mwenyezi Mungu hakumjaalia.
Katika miaka ya hivi karibuni, Bi. Kidude alishirikishwa sana na wasanii wengine katika kazi zao. Miongoni mwao ni Ahmada Amelewa, Fid Q Juhudi za Wasiojiweza.
Mbali na hayo, mashirika mbali mbali yakiwemo ya kibiashara na yale yasiyo ya kiserikali yaliona mvuto aliokuwa nao Bi. Kidude katika jamii, hivyo wakamtumia katika matangazo mbali mbali maarufu likiwa lile la kutokemeza Malaria.
Ni bibi aliyebahatika kusafiri takriban duniani kote, na vilevile katika maisha yake alijinyakulia tuzo lukuki. Miongoni mwa hizo ni ile ya 2005 WOMEX ikiwa ni kutambua mchango wake mkubwa katika tasnia ya muziki.
Katika siku zake za mwisho, Bi. Kidude alikuwa akiumwa, lakini wengi wanahusisha kuumwa kwake na utu uzima aliokuwa nao.
Kifo chake ni pigo kubwa kwa wote, lakini zaidi ni wanamziki wa kizazi kipya waliokuwa wakimuona Bi. Kidude ni nyanya yao.
Source.BBC SWAHILI
No comments:
Post a Comment