Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete ameondoka nchini jioni ya jana, Jumatatu, Oktoba 28, 2013, kwenda London, Uingereza, kwa ziara ya kikazi ya siku nne ambako atahudhuria Mkutano wa Kimataifa wa Serikali Uwazi (Open Government) uliotishwa na Serikali ya Waziri Mkuu wa Uingereza, Mheshimiwa David Cameroun.
Mkutano huo wa siku mbili utafanyika
keshokutwa Jumatano na Alhamisi kwenye Ukumbi wa Queen Elizabeth 2 mjini
London.
Miongoni mwa mambo makuu ambayo
mkutano huo utazungumzia ni Serikali Uwazi na Ajenda ya Maendeleo Baada ya Mwaka
2015 wakati muongo wa utekelezaji wa Malengo ya Maendeleo ya Milenia (Millenium Development Goals) unafikia
mwisho.
Masuala mengine ambayo yatazungumzwa
katika mkutano ambao Rais Kikwete anaambatana na Mawaziri wake watatu ni pamoja
na uwazi katika manunuzi ya umma, uwazi katika mikataba, haki ya kupata habari,
uwazi katika ukaguzi wa fedha za umma, uwazi wa Serikali na vyombo vya habari,
uwazi katika mikataba ya maliasili, uwazi katika maendeleo ya nchi
zinazoendelea.
Mawaziri wanaoambatana na Rais Kikwete
katika ziara hiyo ni Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa
Mheshimiwa Bernard Membe, Waziri wa Sheria na Katiba Mheshimiwa Mathias Chikawe
na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Utawala Bora Serikali ya Mapinduzi, Zanzibar
Mheshimiwa Mwinyihaji Makame.
Rais Kikwete anatarajia kurejea
nyumbani Jumamosi, Novemba 2, 2013.
Imetolewa na:
Kurugenzi
ya Mawasiliano ya Rais,
Ikulu.
Dar
es Salaam.
29
Oktoba, 2013
No comments:
Post a Comment