TANGAZA NASI LEO 0712709630,0756631636 BARUA PEPE gmkojera@gmail.com

Friday 29 November 2013

Kesi za unyanyaji kijinsia kusikilizwa miezi mitatu


Na Gazeti la Tanzania Daima
NAIBU Waziri wa Katiba na Sheria, Angellah Kairuki, amesema kuanzia mwakani kesi zitakazohusiana na ukatili wa kijinsia, mashauri yake yatasikilizwa ndani ya miezi mitatu  hadi kutolewa hukumu.

 Naibu Waziri Angellah Kariuki
Kairuki alitoa kauli hiyo jijini Dar es Salaam jana wakati wa uzinduzi wa kijitabu cha mwongozo wa kuwasaidia wanawake  waliofanyiwa ukatili kilichoandaliwa na Kituo cha Msaada wa Sheria kwa Wanawake na Watoto (WLAC).

Alisema ili kuhakikisha hilo linafanikiwa kutakuwa na vikao maalumu katika mahakama zinazoendesha kesi hizo, hatua ambayo alisema imeafikiwa na nchi zote za Maziwa Makuu.

“Ni kweli kumekuwepo na ucheleweshaji wa kesi hizi, hali inayowafanya walalamikaji kuachana na kesi hizo kwa kuona kuwa wanapotezewa muda wao, ndio  maana kwa pamoja nchi hizo ziliamua  kuja na azimio moja, ili kuona watuhumiwa wa makosa haya wanashughulikiwa mara moja,” alisema.

Pamoja na mikakati hiyo, Kairuki alitoa wito kwa asasi zinazoshughulika na masuala ya kuwatetea kinamama na watoto  kushirikiana na viongozi wa dini ambao wataweza kuwahubiria  waumini wao umuhimu wa kuishi kwa amani na katafuta suluhu ya matatizo kwa amani.

Mwenyekiti wa WLAC, Nakazael Tenga, alisema wakati takwimu za utafiti wa afya  Tanzania ya mwaka 2010 zikionyesha asililimia 39 ya wanawake wote Tanzania wameathirika kwa namna moja au nyingine na ukatili wa kimwili tangu wakiwa watoto, mkoa wa Dodoma umeonekana kuongoza kwa vitendo hivyo kwa asilimia 70.

Mkoa wa Mara ambao awali ulikuwa ukiongoza sasa hivi vitendo vimepungua na kufikia asilimia 66.4, Ruvuma (50.8) na Morogoro (50.1), takwimu ambazo Tenga alisema haziridhishi kwani karibu kila mkoa nchini unakabiliwa na titizo hilo.

Naye Mkurugenzi Mtendaji wa WLAC, Theodosia Muhulo, alisema ipo haja ya kuanzishwa mahakama ya familia ambayo itakuwa ikishughulikia kesi zote zinazohusiana na migogoro ndani ya familia.

No comments:

Post a Comment