TANGAZA NASI LEO 0712709630,0756631636 BARUA PEPE gmkojera@gmail.com

Wednesday, 21 March 2012

Asha Baraka kuwanufaisha vijana 50 wenye vipaji vya kuimba



Mmiliki wa Bendi ya Twanga Pepeta Asha Baraka akiwa katika pozi na tuzo aliyowahi kuipata miaka ya hivi karibuni                                                                                      










Baada ya Bendi ya African Stars kunyakuliwa dansa na mwimbaji wake kwenda katika bendi ya mashujaa hatimaye sasa imeamua kuja kivingine kwa kuhakikisha kwamba inakuwa na bendi nyingine yenye vipaji lukuki.
Mchakato wa kuanzisha bendi ya academy ulianza rasmi mapema mwaka huu ambapo kuna vijana wengi walijitokeza kuchukua fomu ili kuonyesha vipaji walivyonavyo.
Waliojitokeza kusaka  nafasi ni wengi sana lakini zaidi vijana 50 ndio waliopatikana na tayari wameanza kujifua na mazoezi ya kuimba, kupiga muziki na kucheza. Hiyo yote ni katika kuhakikisha kuwa bendi hiyo haiishiwi na vipaji bali kuongeza zaidi ili baadaye hata wanapoondoka wanachukuliwa waliopo kuendeleza kurudumu.
Lengo ni kuhakikisha African Stars Bendi inaendelea kutoa ajira kwa vijana wenye vipaji sio tu waweze kufanya kazi katika bendi hiyo bali pia wanaweza kufanya kazi katika bendi nyingine mbalimbali ikiwa watahitajika.
Katika mazungumzo na gazeti hili Mkurugenzi wa bendi hiyo Asha Baraka ameliambia gazeti hili kwamba kama ilivyo kawaida kwao wamelenga kuwasaidia vijana wenye vipaji  na wenye nia ya kuwa wanamuziki watakaoendeleza muziki wa dansi.
Anasema vijana hao sio tu watakuwa wanaimba bali pia wameanza kujifunza muziki kwa ujumla kwa maana ya kuimba, kupiga gitaa na vyombo vingine pamoja na kucheza.
“Vijana hao wanafundishwa vitu vyote na tayari  wana meneja wao ambaye anawasimamia katika kufanya mazoezi, kwa kweli karibu vijana wote tuliowachukua wana vipaji,”anasema Asha.
Kwa vijana ambao wataonekana kufanya vizuri wengine watafanya kazi na bendi ya Twanga Pepeta ili kukuza zaidi vipaji. Hiyo yote ni katika kuhakikisha wanapata ajira kama ilivyo kwa vijana wengine ambao tayari walikwisha chukuliwa siku zilizopita na sasa wanaendelea kufanya vizuri.
Vile vile, anasema vijana hao watakuwa wakichangamsha katika bendi hasa katika muziki wa dansi ambao unazidi kupendwa kwa kadri miaka inavyozidi kusogea. Ni rahisi kwao kupata kazi hata katika bendi nyingine cha msingi ni kuonyesha jitihada kuzingatia yale wanayofundishwa.
Mama Asha Baraka sio mara ya kwanza kufanya jambo kama hilo, kila mwaka hujitahidi kwa nafasi yake kutafuta vipaji vipya. Mwaka jana alikuwa akitafuta madansa ambapo ilikuwa ikifadhiliwa na manywele na hatimaye kupata mshindi ambaye alichukuliwa na kufanya kazi na twanga pepeta.
Vile vile, anasema siku za nyuma aliwahi kuwachukua vijana kutoka jumba la sanaa THT na wengine walichukuliwa kutoka BSS. Wote wanafanya kazi vizuri na hadi leo wameonekana kung’ara katika anga ya muziki wa dansi.
Katika mitaa mbalimbali tunayoishi kuna vipaji vingi vya kuimba, kucheza na kuchezea vyombo bado hawajulikani. Walikuwa wanatafuta nafasi kama hiyo ili waweze kuonyesha vipaji walivyo navyo. Kwa fursa ambayo mama Asha Baraka amekuwa akiwapa vijana ni dhahiri wengi waliosikia tayari wamejitokeza ili kukuza vipaji vyao.
Ingawa bado kuna wengine wako mikoani na wanatamani kufikiwa na fursa hiyo ila wanashindwa ni kwa vipi watapata ama kupewa nafasi hiyo. Kwa sasa ukichunguza kila nyumba utaona kuna mmoja ana kipaji cha kuimba, na sio rahisi kuwatambua wote kwa mara moja.
Jambo muhimu ni kwamba  wale waliobahatika kupata nafasi hiyo wasiichezee kwa maana kwamba bahati haiji mara mbili, watumie nafasi hiyo kuonyesha jitihada na bidiii ili hatimaye waweze kutimiza ndoto zao.
Mama Baraka anasema hata kwa wale madansa wana nafasi ya kujifunza kuimba na kupiga vyombo ili waweze kudumu hata pale wanapokuwa ni wazee, kwa vile wakibaki katika nafasi moja tu ya kucheza wanapokuwa ni watu wazima watashindwa kufanya kazi hiyo.
“Ninawaambia madansa pia kujifunza kuimba na kushika vyombo kwa manufaa ya baadaye wanatakiwa kufikiria mbele je akizeeka ni nini atafanya ili kuendeleza kipaji chake, wasibaki katika nafasi moja,”anasema.
Hivyo basi madansa wafanye kazi yao kwa kufikiria maisha ya uzeeni yatakuwaje, wawe na ujuzi mwingine ili uweze kuwasaidia baadaye kama ambavyo mama Asha anasisitiza.
Mwisho.

No comments:

Post a Comment