TANGAZA NASI LEO 0712709630,0756631636 BARUA PEPE gmkojera@gmail.com

Monday 2 April 2012

Uigizaji kama huna mfadhili ni ngumu

Moja ya changamoto ambazo hukumbuka vikundi vingi vya uigizaji ni kukosa ufadhili  ambao ungewezesha vikundi husika kutimiza ndoto na malengo waliyojiwekea ya kuendeleza sanaa ya uigizaji ili hatimaye kuwa ajira rasmi kwa vijana wanaotegemea.
Wiki hii nilifanikiwa kukutana na Kikundi kinachojulikana kama Kibaigwa Taijquan ambacho hujihusisha na uandaaji  wa filamu, mchezo wa karate, muziki na ngumi. Ni kikundi ambacho kilianza kazi zake rasmi miaka 9, iliyopita.
Kikundi hicho kiko Mbagala Zakeem katika mtaa wa Kibaigwa ambapo hufanya kazi na vijana mbalimbali wa mtaani  na tayari kuna filamu kama tatu ambazo wameshazitengeneza nyingine zikiwa tayari sokoni na nyingine zikiwa njiani kuelekea sokoni.
Katika mazungumzo na Mratibu wa kikundi hicho Yassin Kanyama anaeleza kuwa licha ya jitihada za kutoa filamu tatu hadi sasa hakuna mafanikio  makubwa waliyoyapata kutokana na mauzo ya filamu hizo.
Filamu ya kwanza waliitoa mwaka 2010 ilikuwa ikijulikana kama ‘The killing of campsite’ ambayo ilichezwa ikiwa na mtindo wa kareti. Walifanikiwa kufanya kazi na Zena Video na fedha walizopata zilikuwa ni kiasi hivyo waliweka katika mfuko wa kuendeleza kikundi.
Filamu ya pili waliitoa mwaka 2011 ilikuwa ikijulikana kama kahaba wa mapenzi ambapo pia mtindo waliotumia ni ule wa kareti, wakati filamu yao ya tatu inaitwa Jitu na ilifanikiwa kufanya vizuri  na kuwatangaza kwa kiasi kikubwa ambapo ilisambazwa na kampuni ya Splash iliyoko chini ya Step na nyingine ambayo iko jikoni inapikwa inaitwa bakora ambapo watamalizia mkataba wao na Splash.
Anasema kwa jinsi ambavyo wanatoa filamu moja ndipo wanapojifunza mambo mengi kwani kila moja hujifunza kulingana na makosa wanayofanya hivyo pia huboresha yale mapungufu ili kutoa filamu ambazo ni nzuri zaidi ya nyingine na kuweza kukubalika katika soko.
Baada ya kugundua kuwa kufanya kazi na Kampuni za usambazaji kunachangia mapato kidogo sana, mipango iliyopo wanataka kuhakikisha wanasambaza wenyewe ili hatimaye waweze kupata faida kwa manufaa yao na kikundi kinachowategemea.
Lakini bado wanatamani wangepata mfadhili mwenye masharti nafuu ili aweze kufanya nao kazi kwani wanaamini wakipata mtu muelewa pengine anaweza kuwakomboa.
Sababu kubwa ya wao kutaka kutafuta mfadhili ni kwa vile bado kipato chao ni kidogo kiasi kwamba wangepata msaidizi ingewaletea nafuu kubwa. Hilo ndilo jambo ambalo wanaliamini zaidi.
Kanyama anasema katika kikundi chao walijiwekea mikakati mingi na mojawapo ni kuhakikisha kuwa wanakuwa na eneo watakalomiliki ikiwa na maana ya kuhamishia ofisi na studio zao ambazo watazianzisha kwa ajili ya kuendeleza vipaji vya uigizaji na fani nyingine wanazozisimamia.
Wapo baadhi ya vijana wako katika kikundi  hicho wameangukia katika sanaa ya muziki lakini bado hawajaweza kutoka kwa vile bado wanakabiliwa na ugumu wa kupata fedha kwa ajili ya kurekodi. Lakini hawajakata tamaa kwani wanaendelea kujipa moyo wakiamini ipo siku watatoka.
Changamoto nyingine wanayokabiliwa ni jinsi ya kupata runinga ili waweze kutengeneza tamthiliya ambazo zitakuwa zinarushwa ili kuelimisha jamii kuhusiana na maisha ya kila siku.  
Anasema wameshazunguka sehemu mbalimbali ili kutafuta runinga lakini tatizo lililopo wanaelezwa watafute mfadhili ili aweze kuwasaidia maigizo yao kurushwa, na kwasababu kipato chao bado ni kidogo walijikuta wakikata tamaa ya kile walichokuwa wanatamani.
“Hatuna mtu wa kutusaidia ili tuweze kufanya yale tunayoyapenda kwa ajili ya kuelimisha jamii, kilichopo tunaangalia kwa sasa tufanyeje ili kazi yetu iweze kukubalika na kuuza wenyewe kwa manufaa yetu,” anasema Manyama.
Hata hivyo, makundi mengi yamekuwa yakianzishwa yakiwa na malengo ya kujikomboa wengi huishia njiani namna hii kwasababu ya kipato. Lakini kwa upande wa kundi hilo linajivunia wachezaji wake kuwa ni wavumilivu licha ya kutonufaika ipasavyo.

No comments:

Post a Comment