TANGAZA NASI LEO 0712709630,0756631636 BARUA PEPE gmkojera@gmail.com

Wednesday 9 May 2012

AFANDE SELE KUTUMBUIZA MIKOA YOTE TANZANIA


Afande Sele akitumbuiza katika moja ya matamasha yake
Msanii Mkongwe wa muziki wa bongo fleva Afande Sele amesema anatarajia kupiga shoo kubwa katika mikoa yote ya Tanzania bara  ili kutoa burudani kwa mashabiki wake na wapenzi wa muziki huo.

Hadi sasa tayari  ameshatoa burudani  katika mikoa ya Lindi na Mtwara. Akizungumza na gazeti hili jana alisema ndani ya wiki hii anatarajia kwenda kuburudisha katika mikoa ya Mbeya, Songea, Iringa na mikoa mingine ambapo atadhaminiwa na Kinywaji cha Pepsi.

Alisema Kinywaji hicho kimemdhamini kupiga shoo mikoani ambapo pamoja na burudani pia April mwaka huu aliteuliwa kuwa Balozi wa Pepsi na kwamba amesaini mkataba wa kufanya  nao kazi hadi Desemba mwaka huu.

“Nashukuru Mungu kinywaji cha Pepsi kimeniteua kuwa Balozi wake na kimenidhamini katika shoo zangu ambapo nitaenda kupiga karibu mikoa yote ya Tanzania, nachosisitiza ni mashabiki mbalimbali kujitokeza pindi tutakapofika mikoani ili kutuunga mkono,” alisema.

Mbali na hilo, Afande Sele kwa mwaka huu tayari ameshatoa wimbo uitwao ‘Mr. President’ ambao umekuwa ukichezwa katika baadhi ya vyombo vya habari. Kinachomsikitisha ni kuona kuwa nyimbo zenye ujumbe zinawekwa pembeni huku zile za mapenzi zikipigwa sana.

Alisema nyimbo zao zimekuwa hazichezwi sana kwenye redio kutokana na chuki binafsi za baadhi ya watu, lakini anachoshukuru ni kuona kuwa kuna watu wanafuatilia kwenye mtandao na kuzisikiliza hivyo anapata moyo wa kuendelea kuimba.

Afande alisema baadhi ya watu wamekuwa wakimuhoji kwamba yuko kimya hasikiki wakati kila mwaka hutoa nyimbo mpya ila tatizo ni baadhi ya watu kutozipiga nyimbo zake jambo ambalo hata mashabiki wake wamekuwa wakiamini pengine ameacha muziki wakati bado yuko sokoni.

No comments:

Post a Comment