TANGAZA NASI LEO 0712709630,0756631636 BARUA PEPE gmkojera@gmail.com

Tuesday 6 November 2012

Tamko la wanawake na katiba


WOMEN FUND TANZANIA (WFT)

P.O.B.O.X 79235 DAR ES SALAAM

 
KONGAMANO JUU YA MASUALA YA HAKI ZA WANAWAKE NA   KATIBA
                                                          TAMKO

Sisi, wanawake kutoka asasi zisizo za kiserikali na mitandao inayoshughulikia masuala ya kijamii kutoka mikoa 19 ya bara na visiwani, tumekutana katika hoteli ya Blue Pearl, Dar es Salaam mnamo Oktoba 22 hadi 24 kujadili haki za wanawake katika Katiba mpya ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Tunatambua kuwa wanawake wanaendelea kuhusishwa katika mchakato wa kukusanya maoni kuhusu Katiba mpya ulioanza mwaka huu. Mkutano huu ni muendelezo wa harakati za kuhakikisha kwamba wanawake wanatoa sauti ya pamoja ya kudai Katiba mpya izingatie masuala ya kijinsia.

 Sisi,wanawake kutoka asasi hizi za kijamii na kitaaluma zipatazo 50, tunatumbua kuwa Katiba inayozingatia masuala ya kijinsia ni ile iliyotokana na mchakato uliyoshirikisha sauti za wanawake na wanaume, na iliyoweka bayana makubaliano ya misingi mikuu itakayoongoza nchi yetu. Vilevile ni Katiba iliyojengewa misingi ya usawa, utu na heshima ya mwanamke na mwanaume inayokataza aina zote za ubaguzi na unyanyasaji wa kijinsia.

 
Sisi, wanawake wa mitandao hii tunasisitiza kuwa mchakato wa mabadiliko ya Katiba mpya ufanyike kwa kutambua kuwepo kwa:

 Ubaguzi wa kijinsia unaoathiri upatikanaji wa haki za msingi za wanawake uliyojikita katika misingi ya ubaguzi wa jinsia.

 Ubaguzi na unyanyapaa dhidi ya walemavu na hususani walemavu wanawake,

 Ukiukwaji wa haki za watoto na ubaguzi wa watoto wa kike, Kwa kuzingatia haya, madai muhimu ya wanawake ni kama yafuatayo:

Katiba ikiri kuwa imetokana na muafaka wa kitaifa uliyopata ridhaa ya mwanamke na mwanaume, hivyo wote wana haki ya kuwa na katiba, kuijua na kuitumia kama sheria mama ya ulinzi wa haki zao.

 

  • Katiba iwe na sura (chapters) maalum zinazoweka bayana haki za wanawake, haki za watoto, na haki za makundi yenye mahitaji maalum.

 

  • Katiba iandikwe kwa lugha nyepesi na ya kueleweka kwa makundi yote, ikiwa ni pamoja na kuzingatia watu wenye ulemavu, na vipengele vyote vizingatie mtazamo wa kijinsia.

 

  • Katiba iunde chombo maalum kitakachosimamia haki za wanawake katika maeneo yote ya kijamii, kisiasa na kiuchumi.

 

  • Katiba ibatilishe sheria zote zinazokinzana na haki za msingi za wanawake na watoto wa kike hususani kubatilisha sheria na mila zote za ubaguzi wa jinsia katika masuala ya ndoa, mirathi, haki za kumiliki.  Kwa mantiki hii, Katiba ibainishe kwa uwazi wajibu wa serikali wa kuchukua hatua zote za kisera na sheria ili kulinda na kuhifadhi haki za wanawake katika maeneo hayo.

 

  • Katiba iwajibishe serikali kutekeleza mikataba yote iliyoridhia kuhusu haki za wanawake na walemavu (CEDAW, CRC, ILO Convention). Mikataba hii itambulike kuwa ni sheria za nchi ili kuepusha ucheleweshaji wa kutafsri au kuruhusu uchakachuaji wa mikataba hii katika sheria za nchi.

 

  • Katiba iweke misingi ya kulinda utu wa mwanamke dhidi ya uonevu na ukatili wa jinsia ndani ya ndoa na kwenye jamii, ikiwa ni pamoja na kukataza ubakaji ndani ya ndoa, kukataza mila zinazomdhalilisha mwanamke, (tohara, kurithiwa bila hiari) na kubainisha haki sawa ndani ya ndoa, kukataza ndoa za utotoni za watoto wa kike. Serikali iwajibishwe kuchukua hatua za kisera na kisheria kuimarisha utekelezaji wa haki hizi.

 

  • Katiba iwajibishe serikali kuchukua hatua za kisera na kisheria kulinda haki za msingi za walemavu, na wazee ikiwa ni pamoja na haki ya kuishi, kuheshimiwa, kupata taarifa, kufikia huduma, na haki ya ajira. Pia Katiba iwajibishe serikali kuchukua hatua za kisera na sheria pamoja na kusimamia utekelezaji wa haki za watoto wa kike na kiume katika masuala ya elimu, huduma kuwafikia walengwa, ulinzi na heshima ya utu wao.

 

  • Katiba ikiri kwamba ardhi ya Tanzania ni mali ya Watanzania - wanawake na wanaume na iwajibishe serikali kuchukua hatua za kisera na sheria zitakazoweka misingi ya kumwezesha mwanamke kumiliki na kunufaika na utajiri huu wa taifa letu kwa njia zifuatazo: (i) kuzuia uuzaji wa ardhi ya familia bila ridhaa ya wanafamilia wote, (ii) kuzuia uporaji wa ardhi unaofanywa na wawekezaji wa ndani na nje  (iii) kuwawezesha wanawake kupata taarifa za kuwekeza katika sekta mbalimbali za taifa, (iv) kuzingatia mchango wa wanawake katika kilimo ikiwa ni pamoja na kulinda haki zao katika sekta hii.

 

  • Katiba mpya ibainishe misingi itakayozuia kuhodhiwa kwa madaraka katika mihimili mikuu ya utawala kwa jinsia moja. Serikali iwajibishwe kuchukua hatua za kisera na sheria ili kuhakikisha wanawake wanashiriki kwa misingi ya haki na kwa uwiano sawa katika uongozi wa mihimili mikuu, ngazi zote za uongozi, na mashirika ya umma na binafsi: kwa mfano,

 

Ø  Taasisi ya Urais, Makamu, Waziri Mkuu, Mwanasheria Mkuu, Spika na Naibu Spika, wakuu wa mikoa na wilaya, bodi za mashirika ya umma, na viongozi wa mashirika haya.

 

Ø  Serikali iwajibishe mashirika binafsi kuzingatia msingi wa usawa.

 

  • Katiba mpya iimarishe haki zilizopo za kufikiwa na kufaidi huduma za msingi kama vile maji safi na salama, uhakika wa upatikanaji wa chakula, makazi bora, elimu, hifadhi ya jamii pamoja na kusisitiza wajibu wa serikali wa kuhakikisha huduma hizi za msingi zinawafikia wanawake wote wa Tanzania.

 

  • Katiba itambue wajibu mkubwa anaobeba mwanamke wakiwemo wanawake walemavu, katika kuendeleza kizazi cha taifa bila kupewa nyenzo na bila ulinzi wa afya yake. Serikali ipewe jukumu la kuchukua hatua za kisera na sheria, kuhakikisha uwekezaji katika afya ya uzazi, pamoja na kuzingatia haki ya mwanamke ya maamuzi ya msingi kuhusu afya ya uzazi na uzazi salama.

 

  • Katiba mpya itambue mchango mkubwa wa mwanamke katika kukuza na kuendeleza kizazi cha taifa, na mchango huu uthaminishwe na kujumuishwa katika mfumo wa pato la taifa.

 

  • Katiba itambue kwamba elimu ni haki ya mwanamke na mwanaume, na iwajibishe serikali kuhakikisha kila raia anapata elimu hadi kikomo cha uwezo wake, na pia kuchukua hatua za kisera na sheria za kuhakikisha utekelezaji huu. Serikali iwajibishwe kuchukua hatua za makusudi za kuhakikisha kuweka mitaala yenye kujenga dhana ya usawa wa wanawake inatekelezwa nchini kote.

 

Imetolewa 24 Oktoba 2012, Dar es Salaam

No comments:

Post a Comment