TANGAZA NASI LEO 0712709630,0756631636 BARUA PEPE gmkojera@gmail.com

Tuesday 6 November 2012

TGNP Yalaani Vitendo Vya Mkuu wa Wilaya ya Handeni

                                  Taarifa kwa vyombo vya habari
 
TGNP Yalaani  Vitendo Vya Mkuu wa Wilaya ya Handeni, Mhe. Muhingo Rweyemamu Vya Kuwakamata Wasichana Waliopata Ujauzito

 Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP), Shirika linalofanya kazi za kutetea  masuala ya kijinsia, haki za wanawake na wasichana ikiwemo haki ya uzazi salama tumeshtushwa na kusikitishwa na kauli iliyotolewa na Mkuu wa Wilaya ya Handeni Mkoani Tanga Ndugu Muhingo Rweyemamu, kuhusu kukamatwa na kufungwa kwa wasichana waliopata mimba kama njia ya kushinikiza watoe majina ya wanaume waliowapa mimba. Habari hizi zimeandikaa katika  gazeti la the Citizen la tarehe 26 Oktoba 2012 na  athari zake  kwa wasichana kuchambuliwa zaidi na gazeti hilo hilo  tarehe 27 Oktoba 2012

 Inasemekana kuwa wasichana mashuleni katika Wilaya ya Handeni wanalazimishwa kupimwa ujauzito na wanapokutwa na ujauzito wanafukuzwa shule. Wasichana hawa hupelekwa polisi kwa mahojiano zaidi endapo watakataa kuwataja wanaume waliowapa mimba. Vitendo hivi vya udhalilishaji  vimetolewa taarifa  kwenye  mikoa mingine ya  Tanzania ikiwemo mikoa ya  Mbeya na Iringa. Swali la kujiuliza ni kwa nini msichana aadhibiwe vikali namna hiyo?adhabu ya kwanza kupata ujauzito akiwa mwanafunzi/umri mdogo, adhabu ya pili anafukuzwa shule/ nyumbani na dhabu nyingine akamatwe na kupelekwa polisi. Tunaelewa kuwa kuna mazingira mengi hatarishi yanayochangia mtoto wa kike kubakwa na kupata ujauzito, ukiwemo umbali wa kutoka nyumbani hadi shuleni,ukosefu wa mabweni,  gharama mbali mbali ikiwemo michango ya shule, mazingira duni ya kujifunzia na kufundishia, ukosefu wa chakula cha mchana, watoto wa kike hushawishiwa kujiingiza kwenye kubakwa na hatimaye kupata ujauzito na kukatishwa masomo.

Mfumo wa elimu yetu ya Tanzania unaendeleza matabaka kwani  wasichana wachache wanakwenda kwenye shule nzuri na kwa gharama kubwa  na hata wakipata ujauzito wanaweza kutoa hizo mimba!!!bali  wasichana walio wengi wanakwenda kwenye shule zisizo na rasilimali za kutosha  hasa maeneo ya vijijini na ndiyo wanaofukuzwa wakipata ujauzito. Mfano katika utafiti wa kiraghbishi uliofanywa na Mtandao wa Jinsia Tanzania mwaka huu kwenye vijiji vitatu vya Kata ya Songwa, Mkoa wa Shinyanga wasichana 38 kwa muda wa miaka 2 walikatishwa masomo kutokana na ujauzito.

 Kutokana na vitendo hivyo vya udhalilishwaji, sisi kama wanaharakati  wa masuala ya usawa wa kijinsia, haki za kibinadamu na demokrasia tumechukizwa  sana na tunalaani vikali vitendo na kauli hii ya mkuu wa wilaya  na tunakemea na kusema  yafuatayo:

 

Madai yetu  kwa Mkuu wa Wilaya ya Handeni  

1.       Kuacha mara moja kuwakamata wasichana wanaopata ujauzito na kuwatoa mara moja wale ambao tayari wamepelekwa jela. Pamoja na kuzindua hiyo KAMPENI ya NIACHE NISOME, atuambie kama imeingizwa kwenye mpango mkakati wa wilaya na umetengewe rasilimali kiasi  gani na za kufanya nini???

2.        Atuweke wazi utaratibu anaotumia kuwawajibisha wahusika kwani kuna taratibu za kisheria zinabidi kufuatwa ili kuwabana na  kama hospitali ya Wilaya ya Handeni ina mashine ya kupima DNA itakuwa Hospitali ya mfano? Je kama  hospitali haina anapaswa kuwajibika??

             Madai yetu  kwa Serikali ya Jamhuri ya  Tanzania

1. Elimu juu ya afya ya uzazi, ikiwemo mbinu za uzazi salama lazima ziwekwe wazi na kufikiwa na wasichana wote na zitolewe bila kuwepo na unyanyapaa wowote

2 .Lazima kuwepo na ulinzi wa kutosha kwa wasichana na haki ya kufikia elimu bora na nafasi za ajira, maisha endelevu na huduma za afya ya uzazi ambazo zinathamini ustawi wa msichana

       3. Sheria ya makosa ya kujamiiana ya mwaka 1998 lazima irekebishwe na kuwepo kipengele kinachotoa si adhabu kali tu kwa wanaume wanaowapa mimba wasichana, bali kiongezwe kipengele cha kuhakikisha matunzo ya mtoto na huyo binti na liwe ni suala la kikatiba

 

Kutokana na kauli ya DC tunatoa wito kwa mamlaka ya serikali ya wilaya ya Handeni na sehemu nyingine popote,ya kuweka mazingira endelevu kwa watoto wa kike kulindwa na kufikia malengo yao bila ya kukandamizwa zaidi. Kuwepo na stadi za maisha za kuwajengea uwezo watoto wa kike ambazo zitawapelekea kuwataja wanaume ambao watawasababishia mimba wakiwa bado watoto.

 

Tunatoa wito kwa wahusika wote na mamlaka za serikali kuchukua hatua za haraka za kutoa elimu ya afya ya uzazi ikiwemo uzazi  salama kwa wasichana na jamii nzima na uingizwe kwenye mitaala ya elimu; kusaidia upanuzi wa usalama wa maisha endelevu kwa wasichana na mazingira rafiki ya kufanyia kazi kwa wote wanawake, wanaume, vijana hasa walioko pembezoni. Tunatoa wito kwa famillia zote, kutoa kipaumbele kwenye mahitaji maalum ya wasichana na kuwapa msaada wanaohitaji katika kufikia elimu bora, afya ya uzazi  salama na  maisha endelevu na yenye heshima.

 

Kamwe haki ya  msichana haikuzwi kwa kumtupa jela ni kwa kumpa elimu bora ili aweze kufikia ndoto yake ya hapo baadae.

 

Imetolewa  Dar es salaam leo 31/10/2012 na

 

 

......................

Lilian Liundi

Kaimu Mkrugenzi Mtendaji TGNP

 

No comments:

Post a Comment