TGNP Yalaani Vitendo Vya Mkuu wa Wilaya ya Handeni, Mhe. Muhingo Rweyemamu Vya Kuwakamata Wasichana Waliopata Ujauzito
Mfumo wa
elimu yetu ya Tanzania unaendeleza matabaka kwani wasichana wachache wanakwenda kwenye shule
nzuri na kwa gharama kubwa na hata wakipata ujauzito wanaweza kutoa hizo mimba!!!bali wasichana walio wengi wanakwenda kwenye shule zisizo na rasilimali za kutosha hasa maeneo ya vijijini na ndiyo wanaofukuzwa
wakipata ujauzito. Mfano katika utafiti wa kiraghbishi uliofanywa na Mtandao wa
Jinsia Tanzania mwaka huu kwenye vijiji vitatu vya Kata ya Songwa, Mkoa wa
Shinyanga wasichana 38 kwa muda wa miaka 2 walikatishwa masomo kutokana na
ujauzito.
Kutokana na vitendo hivyo vya udhalilishwaji, sisi kama
wanaharakati wa masuala ya usawa wa
kijinsia, haki za kibinadamu na demokrasia tumechukizwa sana na tunalaani vikali vitendo na kauli hii
ya mkuu wa wilaya na tunakemea na kusema
yafuatayo:
Madai yetu kwa Mkuu wa Wilaya ya Handeni
1.
Kuacha mara moja kuwakamata wasichana wanaopata ujauzito na
kuwatoa mara moja wale ambao tayari wamepelekwa jela. Pamoja na kuzindua hiyo KAMPENI
ya NIACHE NISOME, atuambie kama imeingizwa kwenye mpango mkakati wa wilaya
na umetengewe rasilimali kiasi gani na za kufanya nini???
2.
Atuweke wazi utaratibu anaotumia kuwawajibisha wahusika
kwani kuna taratibu za kisheria zinabidi kufuatwa ili kuwabana na kama hospitali ya Wilaya ya Handeni ina
mashine ya kupima DNA itakuwa Hospitali ya mfano? Je kama hospitali haina anapaswa kuwajibika??
Madai yetu kwa Serikali ya Jamhuri ya Tanzania
1. Elimu juu ya afya ya uzazi, ikiwemo mbinu za uzazi salama
lazima ziwekwe wazi na kufikiwa na wasichana wote na zitolewe bila kuwepo na
unyanyapaa wowote
2 .Lazima kuwepo na ulinzi wa kutosha kwa wasichana na haki ya
kufikia elimu bora na nafasi za ajira, maisha endelevu na huduma za afya ya
uzazi ambazo zinathamini ustawi wa msichana
3. Sheria ya makosa
ya kujamiiana ya mwaka 1998 lazima irekebishwe na kuwepo kipengele kinachotoa si
adhabu kali tu kwa wanaume wanaowapa mimba wasichana, bali kiongezwe kipengele
cha kuhakikisha matunzo ya mtoto na huyo binti na liwe ni suala la kikatiba
Kutokana na kauli ya DC tunatoa wito kwa mamlaka ya serikali ya
wilaya ya Handeni na sehemu nyingine popote,ya kuweka mazingira endelevu kwa
watoto wa kike kulindwa na kufikia malengo yao bila ya kukandamizwa zaidi. Kuwepo
na stadi za maisha za kuwajengea uwezo watoto wa kike ambazo zitawapelekea
kuwataja wanaume ambao watawasababishia mimba wakiwa bado watoto.
Tunatoa wito kwa wahusika wote na mamlaka za serikali kuchukua
hatua za haraka za kutoa elimu ya afya ya uzazi ikiwemo uzazi salama kwa wasichana na jamii nzima na
uingizwe kwenye mitaala ya elimu; kusaidia upanuzi wa usalama wa maisha
endelevu kwa wasichana na mazingira rafiki ya kufanyia kazi kwa wote wanawake,
wanaume, vijana hasa walioko pembezoni. Tunatoa wito kwa famillia zote, kutoa
kipaumbele kwenye mahitaji maalum ya wasichana na kuwapa msaada wanaohitaji
katika kufikia elimu bora, afya ya uzazi salama na
maisha endelevu na yenye heshima.
Kamwe haki ya msichana
haikuzwi kwa kumtupa jela ni kwa kumpa elimu bora ili aweze kufikia ndoto yake
ya hapo baadae.
Imetolewa
Dar es salaam leo 31/10/2012 na
......................
Lilian Liundi
Kaimu Mkrugenzi Mtendaji TGNP
No comments:
Post a Comment