Waziri Mkuu wa Tanzania Mhe. Mizengo Pinda |
WAZIRI
MKUU AENDESHA HARAMBEE YA PAPO KWA PAPO KUCHANGIA UKARABATI WA VISIMA TISA
WAZIRI MKUU Mizengo Pinda ameendesha harambee ya papo hapo
na kufanikiwa kuchangisha sh. milioni nane kwa ajili ya ukarabati wa pampu za
visima tisa vya maji kwa wakazi wa kijiji cha Magamba, kata ya Magamba wilaya
ya Mlele mkoani Katavi.
Waziri Mkuu alilazimika kuendesha harambee hiyo jana
mchana (Jumapili, Januari 6, 2013) wakati akijibu hoja za wakazi wa kata hiyo
kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika kwenye uwanja wa shule ya sekondari
Magamba wilayani Mlele.
Kaimu Mhandisi wa Maji wa Wilaya hiyo, Bw. Enock Msengi
alisema wanakijiji hao kupitia kamati ya maji walikuwa na sh. 150, 000/- kwenye
akaunti yao. “Kama wangekuwa na fedha walau sh. milioni tatu, tungemudu baadhi
ya gharama, lakini kwa hizi fedha alizochangisha Waziri Mkuu, tunaweza
kukarabati visima vyote na vikafanya kazi… vinavyohitajika zaidi ni vipuri vya
pampu,” alisema mara baada ya mkutano huo.
Akizungumza na wakazi hao, Waziri Mkuu aliwasisitiza
watumie kilimo cha sesa ili kiwe mkombozi wao. Alipowaita mbele ya hadhara
mabalozi wa mashina 18 na kuhoji kila mmoja wao analima ekari ngapi na anatumia
kilimo gani, alibaini kuwa ni balozi mmoja tu ambaye anatumia kilimo cha sesa
na amepanda kwa mistari na kutumia mbolea.
“Hawa wana ekari moja hadi ekari tano lakini wengi wao
mmesikia ni matuta, matuta, matuta hata kwenye karanga wametumia matuta.
Nawasihi sana mwakani kila mmoja atumie kilimo cha sesa kwa sababu kina tija
zaidi kuliko hayo matuta... yanapoteza sehemu kubwa ya ardhi ya kilimo,”
alisisitiza.
Waziri Mkuu ambaye alikuwa anamalizia ziara yake ya jimbo
kwenye kata mbili kati ya 14 zilizobakia wakati wa ziara yake Desemba mwaka
jana, aliwasihi mabalozi hao watumie umoja wa kikundi chao cha kilimo
kuelimishana na akaahidi kuwatafutia majembe ya kukokotwa na ng’ombe ikiwa ni
pamoja na kuwanunulia maksai ili waboreshe kilimo na wawe viongozi wa mfano.
Alipouliza kuna wafuga nyuki wangapi kwenye mkutano huo,
walijitokeza wanane ambao jumla yao walikuwa na mizinga ya asili 34. Yeye
aliahidi kuwapatia mizinga 50 ya kisasa (ya vibao na ya ngazi) ili waboreshe
ufugaji wao.
Waziri Mkuu alitumia fursa hiyo pia kuhimiza ujasiriamali
kwa kuwaunga mkono akinamama wa Magamba ambao wanauza matunda na kuahidi
kuwapatia sh. milioni tano ili ziwasaidie kuboresha biashara zao lakini
akawataka waunde umoja, wachague viongozi na kuchangishana fedha za kianzio.
“Hapa Magamba siyo mbali na Mpanda mjini ambako yako Makao
Makuu ya Mkoa… ninyi mnaweza kuwa chanzo kizuri cha kuwalisha wale watu wa
mjini matunda na mbogamboga kwa sababu ya mabonde mliyonayo, tumieni hiyo fursa
vizuri,” aliwasisitizia.
Mapema, Waziri Mkuu
alikagua shamba la miembe ya kisasa la shule ya sekondari Magamba na kuahidi
kuwaongezea miche mingine 100. Wakati linaanzishwa Desemba 15, 2010, shamba hilo
lilikuwa na miche 80 lakini 11 imekufa na imebakia 69. Wanatarajia kuanza
kuvuna maembe ya kwanza Desemba, mwaka huu.
(mwisho)
IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU,
JUMATATU, JANUARI 07, 2013.
No comments:
Post a Comment