UONGOZI mpya wa Chama cha Netiboli Tanzania (Chaneta) umekabidhiwa vifaa na mali zote za Ofisi hiyo, na uongozi uliomaliza muda wake chini ya Mwenyekiti mstaafu Anna Bayi huku kukiwa hakuna Ofisi.
Makabidhiano
ya vifaa na mali za Ofisi yalifanyika jana katika uwanja mkubwa wa Taifa, huku
viongozi wapya wakiwa na changamoto ya kutafuta Ofisi ya kufanyia kazi zao,
baada ya kuelezwa kuwa Ofisi iliyokuwa ikitumika mwanzo kwa shughuli za Chama
hicho mkataba wake umekwisha.
Kwa mujibu
wa Katibu Mkuu mstaafu wa Chaneta Rose Mkisi alitaja mali alizokabidhi kwa
uongozi mpya kuwa ni pamoja na Gari aina
ya Noah, akaunti mbili moja ikiwa chini ya Chaneta na nyingine ikiwa chini ya
mke wa Waziri Mkuu Tunu Pinda ambazo zote zina kiasi cha shilingi laki 3 kwa
3.
Vifaa
vingine vilivyokabidhiwa ni pamoja na meza mbili, komputa moja, Ups 1, wireless
1, saa ya ukutani, heater, mipira, jezi za netiboli, saa ya ukutani, tuzo
mbalimbali, vikombe vine vya klabu bingwa ambavyo vilikuwa nje ya ofisi na
vifaa vingine mbalimbali.
Akizungumza
wakati anakabidhi vifaa hivyo, Mwenyekiti mstaafu wa Chaneta Anna Bayi alisema
anawashukuru watanzania, viongozi mbalimbali akiwemo mke wa Rais Mama Salma
Kikwete, mke wa Waziri Mkuu Tunu Pinda kwa kuwa mstari wa mbele katika
kuwezesha timu ya netboli taifa kushiriki michezo ya ndani na kimataifa kwa
mafanikio makubwa.
Alisema
viongozi hao wamekuwa wakifanya kazi bega kwa bega na Chama cha Netiboli na
kufanikiwa kupata ubingwa wa pili Afrika
mwaka jana, lakini pia waliweza kusaidia timu ya netiboli kwenda kushiriki
katika mashindano ya kimataifa Singapore mwaka jana.
“Tunawashukuru
watanzania, viongozi wetu wamekuwa wakifanya kazi nasi bega kwa bega katika
kuhakikisha mchezo wa netiboli unafahamika sio tu upande wa Tanzania peke yake
bali pia tumeweza kwenda hadi ngazi ya kimataifa,”alisema.
Bayi alisema
timu ya netiboli ilishika nafasi ya pili katika mashindano ya netiboli Afrika,
lakini pia waliwezesha nchi kushika nafasi ya 11 duniani kutokana na mchezo
huo.
Akipokea
vifaa hivyo, Mwenyekiti mpya wa Chaneta Anna Kibira aliahidi watanzania kuwa
ataendeleza juhudi zilizoachwa na uongozi uliopita, na kuongeza kuwa kama kuna
mabaya atayaacha kama yalivyo.
Hata hivyo,
alisema atazungumza na Baraza la Michezo Tanzania(BMT) ili kumpa mwongozo wa
nini afanye ili aweze kutafuta Ofisi mapema iwezekavyo kwa ajili ya kuanza kazi
haraka.
Chaneta
ilifanya uchaguzi wake mkuu April 20, mwaka huu mjini Dodoma na kupata uongozi
mpya ulio chini ya Mwenyekiti wake Anna Kibira.
No comments:
Post a Comment