TANGAZA NASI LEO 0712709630,0756631636 BARUA PEPE gmkojera@gmail.com

Thursday 26 September 2013

Hakuna biashara ya binadamu katika Tanzania – Rais Kikwete





TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
Hakuna biashara ya binadamu katika Tanzania – Rais Kikwete

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete amesema kuwa hakuna shughuli za biashara haramu ya binadamu inayofanywa katika Tanzania bali barabara za Tanzania na ardhi yake inatumiwa kupitisha biashara hiyo.

Hata hivyo, Rais Kikwete amesema kuwa Serikali yake itaendelea kushirikiana na nchi jirani kuhusu chimbuko la biashara hiyo na katika kuchukua hatua za kukomesha vitendo hivyo haramu.

Rais Kikwete ametoa msimamo huo wa Tanzania leo, Jumatano, Septemba 25, 2013, wakati alipokutana na kufanya mazungumzo na ujumbe wa Shirika la Misaada ya Maendeleo la Marekani la Millennium Challenge Corporation (MCC) ukiongozwa na Mtendaji Mkuu wake, Bwana Daniel W. Yohannes.

Ujumbe huo ulikutana na Rais Kikwete katika Hoteli ya JW Marriott, mjini New York, ambako amefikia kwa ziara yake ya kikazi nchini Marekani na Bwana Yohannes na wenzake walikuwa wanamwelezea Rais Kikwete maendeleo ya ombi la Tanzania la awamu ya pili ya misaada ya maendeleo baada ya kumalizika kwa awamu ya kwanza.

Katika mazungumzo hayo, Bwana Yohannes ametaka kujua hatua ambazo zinachukuliwa na Serikali ya Rais Kikwete kukabiliana na baadhi ya mambo yanayojitokeza kuwa changamoto katika utekelezaji wa miradi ya MCC kupitia Shirika la Tanzania la Millennium Challenge Account Tanzania – MCA (T).

Baadhi ya changamoto ambazo Bwana Yohannes amezitaja ni pamoja na nini kinafanyika kuhusu TANESCO, kuhusu juhudi za kupambana na rushwa na jinsi gani ya kukabiliana na biashara haramu ya binadamu.

Rais Kikwete ametoa majibu ya changamoto zote tatu na kumweleza Bwana Yohannes kuwa biashara haramu ya binadamu haifanyiki wala kuanzia katika Tanzania na kuwa inaanzia Ethiopia, inapitia Kenya, Tanzania, Malawi na kwenda hadi Afrika Kusini.

“Wanakusanya watu katika Ethiopia na kuna mtu anapewa fedha na watu hao wanaokusanywa. Wanakuja Kenya na kuna mtu wa kuwapokea na kuwahudumia, wanakuja Arusha na hatimaye wanaingia Malawi na Afrika Kusini. Katika Tanzania wanapita tu na kuna wakati tulipata kukamata Waethiopia kiasi cha 19,000 na tukawarudisha kwao kwa gharama yetu,” amesema Rais Kikwete na kuongeza:

“Kutoka Ethiopia watu hawa wamekuwa kama mto usiokauka maji. Hivyo, sisi katika Tanzania tunafanywa kama njia ya kupitia tu. Ni kweli wako mawakala lakini kwa hakika biashara hii haifanyiki katika Tanzania. Inafanyika kwingine na nchi yetu inafanywa kama njia tu. Kuna wakati nilipata kuzungumza na viongozi wa Ethiopia na Kenya kuhusu suala hilo lakini bado tutaendelea kulifuatilia.”

Imetolewa na:
Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,
Ikulu,
DAR ES SALAAM.

25 Septemba, 2013

No comments:

Post a Comment