TANGAZA NASI LEO 0712709630,0756631636 BARUA PEPE gmkojera@gmail.com

Friday 25 October 2013

Waziri Mkuu awaonya watanzania wasijilipue

WAZIRI MKUU Mizengo Pinda ameawaonya baadhi ya Watanzania wengi wanaokuja katika jiji la Guangzhou nchini China kwa ajili ya kununua bidhaa mbalimbali waache kuuza hati zao za kusafiria kwa raia wa nchi nyingine kama njia ya kujiongeza kipato.


Ametoa  onyo hilo jana usiku (Alhamisi, Oktoba 24, 2013) wakati akizungumza Watanzania wanaofanya biashara na wale wanaoishi katika jiji la Guangzhou, jimbo la Guangdong ambalo ni jiji kubwa la biashara lililoko kusini mwa China.


Alisema kuwa wengi wa wafanyabiashara hao wanapouza pasipoti zao wanasingizia kuwa zimepotea ndio maana kuna malalamiko mengi kutoka kwa Watanzania wanaofika katika jimbo hilo kudai wanaibiwa hati zao za kusafiria wakati sio kweli.


Wakati wa mazungumzo hayo, mmoja wa Watanzania hao aliyejitambulisha kwa jina la Ambrose Lugai  alisema changamoto nyingi zinazowakabili Watanzania waishio katika jimbo hilo na moja ya tatizo hilo ni kuibiwa kwa hati za kusafiria za Watanzania.


Bw. Lugai alisema tatizo la wafanyabiashara wengi kupoteza pasipoti limekuwa sugu na kila siku linaongezeka na cha ajabu linawatokea wafanyabiashara wa kutoka Tanzania tu.


“Hatuwezi kusema ni u-carelessnes, lakini jamii ya hapa ni kutoka mataifa mbalimbali, inakuwaje pasipoti za Tanzania tu ndio zinakuwa hot cake, naomba utusaidie namna ya kulinda hati hizi,” alisema Bw. Lugai.


Alimwomba Waziri Mkuu awasaidie kuzungumza na Serikali ya jimbo hilo ili Watanzania wawe wanaacha pasipoti hotelini wakati wanapoenda mitaani, badala yake wapewe karatasi nyingine ya kuwatambulisha huko mitaani.


Katika kujibu hoja hiyo ya Bw. Lugai, Waziri Mkuu alisema kwamba suala hilo linamshangaza kwamba inakuwaje hati za wafanyabiashara wa Tanzania tu ndio zinaiibiwa wakati wafanyabiashara wanaofika kwenye jimbo hilo ni wengi kutoka mataifa mbalimbali. “Kupoteza pasipoti ni jambo la nadra sana, sio la kawaida. Nilitegemea hili linaweza kumtokea mtu mmoja mmoja, lakini nashangazwa kwamba hapa Goangzhou ni tatizo kubwa.”


“Lakini taarifa nilizo nazo nyie wenyewe wafanyabiashara mnauza hati zenu kwa Wanaigeria ili mpate fedha za kufanyia biashara. Ndio maana nawasihi achani haya mambo, mnajifedhehesha wenyewe na mnaifedhehesha nchi,” alisema Waziri Mkuu.


Alisema kwa kuwa tatizo hilo ni kubwa na akamtaka balozi wa Tanzania nchini China, Luteni Jenerali mstaafu Abdulrahman Shimbo afuatilie kwa karibu kujua idadi ya watu walioibiwa hati zao za kusafiria ili Serikali iweze kulishughulikia.


“Lakini nawaonya acheni tabia mbaya ya kuuza pasipoti zenu kwa tamaa ya kupata vijipesa vidogo vidogo hivyo, hii ni kuivunjia nchi heshima,” alisema.


Lakini pia alitaka jumuiya ya Watanzania waishio China kuimarishwa zaidi ili wawe na uwezo wa kushughulikia kero zao mbalimbali zinazowakabili wakiwa katika ugenini. Alisema ni kuimarika kwa jumuiya hiyo tu kutawasaidia wanafunzi na wafanyabiashara kufikisha malalamiko yao haraka serikalini.  



IMETOLEWA NA:

OFISI YA WAZIRI MKUU,
IJUMAA, OKTOBA 25, 2013

No comments:

Post a Comment