Rais Jakaya Kikwete |
Dodoma:Rais Jakaya Kikwete amesema Tanzania haitajitoa katika Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC), licha kuwapo kwa vitendo alivyoviita vya ubaguzi vinavyofanywa na wakuu wa nchi za Uganda, Kenya na Rwanda.
Rais Kikwete akilihutubia Bunge jana mjini Dodoma
alifichua kwamba sababu kubwa ya viongozi hao kuonekana kama wanaitenga
Tanzania ni msimamo wake kuhusu masuala ya Shirikisho la Kisiasa,
Uhamiaji, Ardhi na Ajira.
Rais alikuwa akirejea matukio ya hivi karibuni ya
marais wa Kenya, Uhuru Kenyatta, Uganda, Yoweri Museveni na Rais wa
Rwanda, Paul Kagame kukutana na kujadiliana kuhusu masuala kadhaa
yanayohusu EAC bila Tanzania kuwapo.
“Hatuna mpango wa kuondoka, tupo na tunaendelea
kuwepo na napenda niwahakikishie kwamba Tanzania haijafanya jambo lolote
baya kwa jumuiya yetu au kwa nchi mwanachama mmoja mmoja na tumekuwa
waaminifu na watiifu kwa jumuiya wakati wote,”alisema Rais Kikwete.
Aliwashutumu viongozi wao akisema kuwa kauli zao
kwamba wanakutana kwa sababu wako tayari ni za kibaguzi kwani katika
mikutano yote waliyoifanya Entebbe nchini Uganda, Mombasa – Kenya na
Kigali nchini Rwanda hawakuwahi kuialika Tanzania.
“Hali hii haijawahi kuwapo na ni kwa mara ya
kwanza tunaanza kuwa na makundi ndani ya jumuiya yetu; huku Kenya,
Uganda na Rwanda, kule Tanzania na Burundi,”alisema Kikwete katika
hotuba yake iliyochukua saa1:15 na kuongeza:
“Ikiwa itakuja kutokea jumuiya ikadhoofika au
ikafa, Mungu apishilie mbali Tanzania isije ikanyooshewa kidole kwamba
ndiyo chanzo cha kudhoofika huko au kufa huko”.
Alisema ataendelea kuzungumza na viongozi wa nchi
hizo, na kwamba tayari ameanza ili kuhakikisha utekezaji wa mambo yote
ndani ya Jumuiya ya Afrika Mashariki unafanywa kwa kuzingatia mkataba
ulioanzisha jumuiya hiyo.
Rais Kikwete alisema kwa mujibu wa mkataba huo
mambo yote yanapaswa kutekelezwa kwa kuzingatia kalenda ambayo inaweka
bayana mambo hayo kuwa ni Umoja wa Forodha, Soko la Pamoja, Umoja wa
Sarafu na hatimaye Shirikisho la Kisiasa.
Alisema licha ya kuwapo kwa mambo hayo kwenye
mkataba ambao umesainiwa na nchi wanachama, Kenya, Uganda na Rwanda
wamechukua baadhi ya mambo ambayo kimsingi ni ya jumuiya na kuanza
kuyaweka chini ya himaya yao.
Aliyataja mambo hayo kuwa ni Umoja wa Forodha na
Shirikisho la Kisiasa ambayo taarifa zake zilipaswa kuwasilishwa katika
Mkutano wa Wakuu wa Nchi uliopangwa kufanyika Kampala, Uganda, Novemba
30 mwaka huu.
Kuhusu Umoja wa Forodha, Rais Kikwete alisema
walikubaliana kwamba bidhaa zitozwe ushuru pale zinapoingizwa tu na
baadaye kuwepo utaratibu wa nchi iliyotoza ushuru husika kwenda katika
nchi ambayo bidhaa hizo zinapelekwa, lakini kabla ya utekelezaji
waliwaagiza mawaziri kuandaa utaratibu mwafaka.
No comments:
Post a Comment