TANGAZA NASI LEO 0712709630,0756631636 BARUA PEPE gmkojera@gmail.com

Friday 15 November 2013

Mashirika yasiyo ya kiserikali yaweza kuleta amani ya kudumu

 Na Isaac Mwangi,EANA
 Bujumbura, Novemba 15, 2013 (EANA) - Kushirikisha mashirika yasiyo ya kiserikali katika juhudi za kutafuta suluhisho la miggoro  ya kikanda kunaweza kuimarisha majadiliano na uvumilivu katika kanda ya Afrika Mashariki.

Hayo yalisemwa na Makamu wa Kwanza wa Rais wa Burundi, Bernard Busokoza alipokuwa anafungua mkutano wa pili wa Amani na Usalama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) unaofanyika mjini Bujumbura, Burundi.

Alisema juhudi zinazofanywa za kuleta amani mara nyingi hushughulikia sababu za migogoro husika badala ya vyanzo vyake.

''Ni mara chache sana kwa wadau kuhusishwa na mara nyingi pia suluhisho la migogoro huwa ni maagizo kutoka nje na kutumika kwa pande zote zinazohusika,'' alisema.

Busokoza alisema mkutano huo utasaidia kujenga uwezo wa pamoja wa kutatua migogoro kwa kwa wajumbe.

''Mkutano huu utatoa fursa kwa wadau wote wakiwemo wa umma,binafsi, jeshi,polisi na raia kushiriki kikamilifu katika kujenga uwezo wa kudumu wa kushughulikia masuala ya amani na usalama katika Jumuiya ya Afrika Mashariki na nje ya jumuiya hiyo,'' alifafanua.
  
Akihutubia wajumbe katika mkutano huo pia, Waziri katika Ofisi ya Rais anayeshughulikia EAC, Leontine Nzeyimana alisema hatua maalum zinahitajika kubaini na kuzuia vitisho dhidi ya amani na shughuli za kigaidi.'' Tunahitaji kuimarisha mitandao yetu ya kiintelejensia ili kukabiliana vitisho hivyo.''

Naye Naibu Katibu Mkuu wa EAC anayeshughulikia Shirikisho la Kisiasa, Charles Njoroge alitoa wito kwa wajumbe wa mkutano huo kuleta mapendekezo ya namna kanda hiyo kwa pamaja itakavyoweza kukabiliana na vitisho vya kutoweka kwa amani na usalama badala ya kuingia katika migogoro.

Mkutano huo unahudhuriwa na wajumbe 150 kutoka nchi wanachama wa EAC, ikiwa ni pamoja na Kenya, Uganda, Tanzania, Burundi na Rwanda. Umeandaliwa kwa ushirikiano kati ya Sektretarati ya EAC na Shirika la Misaada la Kimataifa la Ujerumani (GIZ).

IM/lC/MM/NI

No comments:

Post a Comment