THE UNITED
REPUBLIC OF TANZANIA
DIRECTORATE OF
PRESIDENTIAL COMMUNICATIONS
Telephone:
255-22-2114512, 2116898
Fax: 255-22-2113425 |
|
PRESIDENT’S OFFICE,
THE
STATE HOUSE,
P.O. BOX 9120,
DAR
ES SALAAM.
Tanzania.
|
TAARIFA
KWA VYOMBO VYA HABARI
Rais wa
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete amewasili
mjini Colombo, Sri Lanka, leo, Alhamisi, Novemba 14, 2013, kuhudhuria Mkutano
wa Wakuu wa Serikali za Nchi Wanachama wa Jumuiya ya Madola (CHOGM).
Rais Kikwete
ambaye anaandamana na Mama Salma Kikwete amewasili mjini Colombo, mji mkuu wa
Sri Lanka, asubuhi ya leo, akitokea Dubai ambako aliwasili usiku wa jana
akitokea nyumbani.
Mkutano huo wa
siku tatu unaanza kesho, Ijumaa, Novemba 15, 2013, kwenye Ukumbi wa Mahinda
Rajapaska Theatre katika eneo la Nelum Pokuna mjini Colombo, mji mkuu wa Sri
Lanka.
Mkutano huo
utafunguliwa rasmi na Prince Charles, mtoto wa Malkia wa Uingereza, kwa niaba
ya mama yake, Malkia Elizabeth ambaye ndiye kiongozi wa Jumuiya ya Madola,
ambaye hata hivyo, hataweza kuhudhuria mkutano wa mwaka huu.
Mara baada
sherehe za ufunguzi, Rais Kikwete ataungana na viongozi wenzake kwa ajili ya
vikao rasmi vya mkutano huo vitakavyofanyika kwenye Kituo cha Maonyesho ya
Kumbukumbu cha Sirimavo Bandaranaike.
Miongoni mwa
shughuli kubwa za kesho ni vikao viwili rasmi vya kwanza vya viongozi wa Jumuiya
hiyo na majadiliano kati ya viongozi hao na viongozi wa vijana kutoka nchi
wanachama wa Jumuiya ya Madola.
Aidha,
viongozi hao wa Jumuiya ya Madola akiwamo Rais Kikwete watahudhuria hafla rasmi
ya makaribisho itakayoandaliwa na Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Madola, Mheshimiwa
Kamalesh Sharma katika Ukumbi wa Bandaranaike Memorial International Conference
Hall (BMICH).
Baadaye leo,
Rais Kikwete na Mama Salma, watahudhuria Hafla ya Chakula cha Usiku
kitakachoandaliwa na Prince Charles na mkewe, The Duchess of Corwall, kwenye
Hoteli ya Cinnamon Lakeside.
Jumuiya ya
Madola ni umoja wa nchi zilizokuwa chini ya ukoloni na himaya ya Uingereza na
nchi nyingine ambazo zenyewe ziliomba na kukubaliwa kujiunga na Jumuiya hiyo ikiwamo
Mozambique na Rwanda.
Jumuiya ya
Madola ina jumla ya nchi wanachama 53, zikiwamo nchi 18 za Afrika ambalo ni
Bara lenye wanachama wengi zaidi katika Jumuiya hiyo, nchi nane za Asia, nchi
13 za Marekani na Caribbean, nchi tatu za Ulaya na nchi 11 za Pacific.
Jumuiya hiyo
pia ina mchanganyiko wa nchi kubwa na ndogo, nchi 32 kati ya hizo zilihesabiwa
kama nchi ndogo kwa maana ya kuwa idadi ya watu milioni 1.5 ama chini ya hapo.
Sri Lanka
ambayo mpaka mwaka 1972 ilijulikana kwa jina la Ceylon, inajulikama rasmi kama
Jamhuri ya Kidemosia ya Kisoshalisti ya Sri Lanka. Ni nchi kisiwa kilichoko
kaskazini mwa Bahari ya India na Kusini mwa pwani ya nchi ya India. Ni nchi
yenye mipaka ya maji na India na Maldives.
Imetolewa
na;
Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,
Ikulu,
DAR
ES SALAAM.
14 Novemba, 2013
No comments:
Post a Comment