TANGAZA NASI LEO 0712709630,0756631636 BARUA PEPE gmkojera@gmail.com

Wednesday 15 January 2014

Tukumbuke jinsi ambavyo Professa Jay alivyovuma


“Jina langu limevuma, kwenye mitaa. Jina langu lina hadhi ya ki-superstar.Jina langu linaongeza idadi ya maadui, jina langu…..” Hayo ni maneno kutoka kwenye wimbo wa Jina Langu wa msanii mahiri wa Hip Hop  nchini Joseph Haule ‘Professa Jay’.
 
Bila shaka wimbo huu ulimvumisha sana miaka saba iliyopita, ndio maana nimeweza kuyambuka mashairi yake hayo, na bado ni msanii mkongwe anayeendelea kukubalika na anayejivunia mafanikio mengi yaliyotokana na muziki wake.
 Wakati anaanza muziki alikuwa ana ndoto nyingi  ikiwa ni pamoja na kumiliki nyumba, gari, studio kubwa ya kisasa na kuwekeza kwenye ujasiriamali mwingine.
 
Tayari amefanikiwa kwa asilimia kubwa na hiyo yote ni kwasababu ya juhudi zake katika kuhakikisha anatoa muziki utakaoendelea kumweka kwenye chati ya muziki wa kizazi kipya  na kuwavutia maelfu ya mashabiki wake.

Ndani ya mwaka jana ameweza kufungua studio, saluni na tayari anaishi katika nyumba yake ya kisasa iliyoko Kimara Mbezi, jijini Dar es Salaam.

Anasema ilikuwa ni kama ndoto na sasa imekuwa kweli, ni studio ambayo ameiita kwa jina la kilugha yaani  ‘Mwanalizombe studio’  akiwa na maana ya mwana Ruvuma, kwani asili yake ni mkoani humo.

Kama ilivyo kwa wanamuziki wengine nchini, lengo lake kubwa lilikuwa ni kukuza muziki wa kizazi kipya hasa ikizingatia kwamba  ndio unaokuwa na kukubalika kwa kasi kwa kadri miaka inavyosogea.
 

Anasema studio hiyo itatoa nafasi kwa wasanii tofauti tofauti wakiwemo pia wasanii chipukizi kurekodi kazi zao ikiwa ni sehemu ya kukuza vipaji vipya vinavyozaliwa kila siku.

Toka aifungue mwaka jana tayari ameajiri produza mmoja anayemwamini na mwaka huu ataendelea kuboresha baadhi ya mambo muhimu yanayohitajika katika studio hiyo.

Anasema kwanza studio hiyo itawarekodia vijana kwa bei ambayo kila mmoja ataimudu sio kwa ajili ya kukomoa kama ambavyo wengine wamekuwa wakifanya.

Pamoja na studio hiyo, alifanikiwa kufanya uwekezaji kwa kufungua saluni kubwa ya kisasa ambayo ameajiri vijana wengi wa kitanzania wenye ujuzi. Hiyo yote ilikuwa ni mipango aliyojiwekea na kufanikiwa kutimiza.

Anasema ataendelea kuwekeza kwenye mambo mengi zaidi kwani sio kwamba ataendelea kuimba muziki hadi uzeeni, akiamini utamsaidia kuendesha maisha yake na familia yake inayomtegemea huko baadaye.

Yapo mengi ambayo ameyafanya kama sehemu ya mafanikio katika muziki wake ikiwa ni pamoja na kujenga nyumba ya kisasa huko Kimara Mbezi nab ado ana ndoto ya kuendelea kuboresha muziki wake ili asirudi nyuma kama ilivyotokea kwa baadhi ya wanamuziki wakongwe wanaoendekeza starehe zaidi kuliko uwekezaji.

Aliahidi kutoa nyimbo mbili mwezi huu ili kuwarudisha mashabiki wake kwani amekuwa kimya kidogo ingawa kwa mwaka jana alipata shoo nyingine kwenye mikoa mbalimbali kwa kushirikiana na nguli mwenzake Judith Wambura ‘Lady Jaydee’.

Historia yake
Bila shaka kuna baadhi ya watu  hawajapata historia ya msanii huyu wa siku nyingi. Professa Jay alizaliwa miaka 39 iliyopita  jijini Dar-es-salaam. Ni mtoto wa sita kati ya watoto tisa wa Mzee Leonard Steven Haule na Mama Rose Majanjara aliyefariki dunia mwaka jana kwa ajali ya gari. 

Alianza kuimba muziki wa kizazi  kipya mwaka 1990 mara baada ya kumaliza masomo yake na mwaka 1992 ndipo alipoanza kuvuma rasmi.

“Nakumbuka    mwaka 1992 nikiwa  pamoja na mshikaji wangu   KILLA B pale Chuo Kikuu cha Dar es salaam ukumbi wa UDASA. Nakumbuka watu walikuwa kibao na nilikonga sana nyoyo za mashabiki wa muziki huu kwa style yangu ya enzi hizo ya Tongue Twist,”alisema hayo wakati huo ilikuwa ni mara yake ya kwanza kupanda jukwaani.

Prof. Jay anatazamika kama msanii aliyeweza kuwateka wazee waweze kusikiliza muziki wake  hasa kwa kibao alichofanya wakati yupo na kundi la Hard Blasters Crew kilichofahamika kama  Chemsha Bongo.

Ndilo kundi aliloanzia na ilikuwa  ni moja ya makundi yaliyofanya muziki huu ambao hujulikana kama 'muziki wa kizazi kipya' kukubaliwa na sehemu kubwa ya watanzania.

Mwaka 1995 kundi hilo  lilishinda kuwa kundi bora la Hip Hop. Walitoa albamu ya kwanza iitwayo 'Funga Kazi' mwaka 2000. Ndio iliyoleta  mapinduzi makubwa sana ya muziki wa Hip Hop nchini.

Ilikuwa na nyimbo kali zilizovuma wakati huo  'Chemsha Bongo' na 'Mamsapu' ambazo zilichangia kufanya muziki  wa aina hiyo  kuwa wa kila rika na kupewa heshima. Kabla ya hapo muziki huu ulionekana kuwa ni muziki wa wahuni.

Baadaye  aliamua kuwa msanii binafsi mwaka 2001 na  muda mfupi baada ya hapo akatoa albamu yake ya kwanza iitwayo "Machozi Jasho na Damu".

 Albamu hii ilivuma haraka sana na kumfanya kupata tuzo ya kuwa mtunzi bora wa Hip Hop kwa nyimbo yake ya 'Ndio Mzee' ikifuatiwa na Nyimbo ya "Piga Makofi na Bongo Dar es Salaam zote zilitikisa wakati huo.

Mwaka 2003  alitoa albamu ya pili iitwayo "Mapinduzi Halisi" ambayo nayo ilishinda tuzo ya Kili Muziki awards na  kuwa albamu bora ya muziki wa Hip Hop nchini. Ilibeba nyimbo kama "Zali la Mentali", "Msinitenge," na "Promota Anabeep"

Mwaka 2005  alitoa albamu ya tatu iliyoitwa "J.O.S.EP.P.H". Jina la albamu hii lilitokana na nyimbo iliyotoka mwanzo kabla ya kutoa albam hiyo. Nyimbo hiyo ilichaguliwa kuwa bora ya bongo fleva kwenye Shirika la Utangazaji la BBC na Radio One awards 

Pia, imewahi kuteuliwa kuwa ni albamu bora ya Hip Hop ,Mtunzi bora wa nyimbo za Hip Hop, na  wimbo  bora ya Hip Hop  kwenye Kili Music Awards wakati huo kupitia wimbo wa ‘Nikusaidieje’ na baadae Kisima muziki awards ya Kenya  ikiwa ni nymbo bora ya hip hop na Video bora ya Hip Hop kutoka nchini Tanzania.

Mwaka 2011 alitoa albam nyingine  iliyoitwa Jaysco Dagama ilikuwa na nyimbo kama Kamili gado na nyingine kibao.  Anajivunia toka  ameanza muziki zaidi ya miaka 20 iliyopita amefanya shoo kwenye nchi za Marekani, Canada, Ujerumani, Ugiriki, Norway, Sweden, nchi za Afrika Mashariki, Afrika Kusini,  India, Nigeria, Ghana, Ehtiopia , Uingereza na nyingine nyingi.

Pia, ni balozi wa malaria. Mwaka huu amepania kuendeleza mapinduzi katika muziki wake kwa kutoa vitu vikali ili jina lake liendelee kuvuma kwenye mitaa.

No comments:

Post a Comment