Mwanamume raia wa Kenya
anayeshabikia klabu ya soka ya Uingereza ya Liverpool amedungwa kisu na
mwenzake wa klabu ya Arsenal na kufariki dunia katika eneo la Meru
Mashariki mwa Kenya.
Shabiki wa Arsenal anayefanya kazi ya Boda Boda alitajawa na hasira baada ya timu yake kukemewa na shabiki wa Liverpool kiasi cha kumdunga mwenzake kisu mara kadhaa, kabla ya kutoweka.
Watu waliokua karibu na eneo la tukio hilo walimsaidia mwathiriwa aliyetambuliwa kama Anthony Muteithia na kumpeleka katika hospitali kuu ya Meru ambapo alifariki dunia wakati akipokea matibabu.
Mkuu wa polisi eneo la Meru Tom Odero amesema wanamsaka shabiki huyo wa Arsenal ambaye amekwenda mafichoni.
Hapo Disemba mwaka jana shabiki wa klabu ya Manchester United nchini Kenya kwa jina Jimmy Macharia alijiua baada ya klabu hiyo kuendelea kuorodhesha matokeo mabaya.
Na mnamo mwaka 2012 Suleiman Alfonso Omondi shabiki wa Arsenal alijitia kitanzi baada ya timu hiyo kushindwa kwenye mechi. Ligi ya Premia nchini Uingereza huvutia ushabiki mkubwa nchini Kenya na Afrika Mashariki kwa ujumla.
No comments:
Post a Comment