Wajumbe wa Mkutano kati ya Utepe Mweupe na Waziri Mkuu Mizengo Pinda wakiwa katika picha ya pamoja mara baada ya kumalizika kwa mkutano huo Ikulu. |
MUUNGANO wa Utepe Mweupe (White
Ribbon Allience for Safe Motherhood Tanzania) wiki hii walikutana na Waziri
Mkuu wa Tanzania, Mizengo Pinda na kujadiliana namna ya Serikali inavyoweza
kuokoa maisha ya wajawazito hasa wakati wa kujifungua.
Pia mkutano huo ulirejea ahadi
ambazo zilishatolewa na serikali kwamba kufikia mwaka 2015 asilimia 50 ya vituo
vyote vya afya nchini Tanzania vitakuwa vinatoa huduma za dharura zikiwemo
upasuaji na damu salama kwa ajili ya kusaidia wajawazito nyakati za kujifungua.
Kupitia kampeni ya ‘Wajibika Mama
Aishi’ iliyochini ya Muungano wa Utepe Mweupe inayolenga kuikumbusha Serikali
ahadi yake ya kuhakikisha asilimia 50 ya vituo vya afya vinatoa huduma za
dharura; walimuomba Waziri Pinda atoe agizo kwa Serikali kuweka kipengere cha
huduma za dharura katika vituo vya afya na kutengewa bajeti mahususi kwenye
bajeti ya Serikali ya mwaka 2014/15.
Takwimu zinaonesha kwa Tanzania kila
siku wanawake 24 hupoteza maisha kutokana na matatizo ya uzazi. Lakini wanawake
wengi wanaopata matatizo yanayosababisha kupoteza maisha, wangeweza kuokolewa
pale tu wanapopata huduma za uzazi za dharura. Njia pekee ya kuepusha vifo
visivyo vya lazima vitokanavyo na matatizo ya uzazi ni wanawake kupata kwa
wakati huduma za dharura kama vile upasuaji na damu salama katika vituo vya
afya wanakojifungulia pale inapobidi.
Katika Mkutano huo, Mkurugenzi wa
Shirika la Evidence For Action Tanzania, Craig Ferrah alisema vifo 24 vya akina
mama vinavyotokea kila siku nchini haina tofauti na ajali za kila siku za ndege
na kuongeza kuwa ipo haja ya Serikali kuweka kuweka mkakati wa kukomesha ajali
hizo ndani ya saa 48.
Hata hivyo ombi kuu kutoka muungano
huo kwa Waziri Mkuu lilikuwa Serikali kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu Tawala za
Mikoa na Serikali za Mitaa iagize kuwepo wa kipengele mahususi cha bajeti ya
huduma za uzazi za dharura zikiwemo upasuaji na damu salama katika vituo vya
afya kwenye bajeti ya mwaka 2014/2015.
Kwa upande wake Waziri Mkuu Pinda aliguswa
na ukubwa wa tatizo hilo la vifo vya wajawazito nchini na kuelezea umuhimu wa
kutafutia namna ya kukabiliana na tatizo ambalo linaelekea kuwa la kudumu.
Waziri Pinda aliridhia moja kwa moja
ombi kutokana na kuguswa na takwimu zilizotolewa juu ya vifo vya wajawazito na
kukubali kuwa Serikali itatenga bajeti mahususi ambayo itaelekezwa kuhimarisha
vituo vya afya nchini ili viweze kutoa huduma ya dharura yaani damu salama,
upasuaji pamoja na wataalamu na vifaa kupunguza vifo vitokanavyo na uzazi.
Mkutano huo pia ulihudhuriwa na
wawakilishi kutoka mashirika ya; Jhpiego, CARE, Plan International (Wazazi na
Mwana), Evidence4Action, Medical Women Association of Tanzania na Chama cha
Wakunga Tanzania walihudhuria kama sehemu ya Muungano wa Utepe Mweupe (White
Ribbon Allience for Safe Motherhood Tanzania).
No comments:
Post a Comment