TANGAZA NASI LEO 0712709630,0756631636 BARUA PEPE gmkojera@gmail.com

Tuesday 17 April 2012

Bushoke kuimba na baba yake Afrika ya Kusini



Mwimbaji mkongwe wa muziki wa bongo fleva Bushoke amekuja tena kivingine kwa kuamua kurekodi nyimbo zake tatu nchini Uganda akiwa amewashirikisha wasanii mbalimbali wa nchini humo.

Nyimbo zake tatu mpya ambazo hupigwa zaidi katika runinga mbalimbali nchini zinajulikana kama bingili, nakupenda na mama wa nghamba ambazo amejaribu kuwashirikisha wasanii mbalimbali wa Uganda wakiwemo Ngoni. Zote hizo zitaingia katika albam yake mpya itakayoitwa katerero.

Akizungumza kwa njia ya simu na blog ya jamii Bushoke alisema katika albam yake hiyo itakuwa na nyimbo kumi ambapo nyingine atashirikiana kuimba na baba yake mzazi Maximilian Bushoke nchini Afrika ya Kusini.

Alisema nyimbo ambazo zimebakia atarekodi katika studio ya baba yake huko Afrika ya Kusini inayoitwa Bushoke records na kwamba kwa sasa wameona ni bora wafanye kazi  kwa pamoja , kwa vile pia baba yake alishawahi kuimba muziki kwa muda mrefu siku za nyuma. 

Msanii huyo ambaye alivuma sana miaka michache iliyopita na nyimbo zake kama Mume bwege, barua na nyimbo nyingine kadhaa amekuwa na mvuto mkubwa kwa mashabiki wengi wa Tanzania kutokana na uimbaji wake wenye ujumbe kwa jamii.

Kama ambavyo inajulikana kwamba mashabiki wengi walianza kumtambua katika anga ya muziki baada ya kutoa wimbo ‘mume bwege’ akijaribu kutoa ujumbe kwa jamii jinsi ambavyo baadhi ya wanaume wakitendewa ubaya na wake zao kwa kugeuzwa kuwa bwege.
Lakini unajua ni kwanini msimu huu ameamua kurekodi muziki wake nje ya Tanzania? Anataka kuhakikisha anatimiza ndoto za kuufanya muziki wake utambulike sio tu katika ukanda wa Afrika Mashariki bali pia katika ukanda wa Kimataifa.

“Unajua nataka nitimize malengo yangu ya kuhakikisha kuwa muziki ninaoimba unafika mbali ndio maana pia nimeamua kushirikiana na wanamuziki wa kimataifa ili kuleta ladha tofauti,”.

Kuna nyimbo mbili Bushoke ameziimba kwa kuchanganya lugha mbili yaani Kiswahili na Kiganda. Hivyo anaamini kuwa muziki wake utaendelea kupendwa na mashabiki mbalimbali kama ilivyokuwa kwa nyimbo zake ambazo tayari ameshazitoa siku za nyuma.

Anawaeleza mashabiki wake kuwa wakae mkao wa kula kwani muziki anaouleta safari hii una vionjo tofauti. Amejaribu kuimba kwa lugha mbalimbali ili ujumbe uweze kuwafikia wengi.

“Mashabiki wangu nawapenda sana na naamini mtanipokea vizuri katika muziki wangu ambao tayari nimeanza kuutoa, nataka niwaletee mambo mazuri ili muweze kuburudika,”anasema.



No comments:

Post a Comment