TAARIFA
KWA VYOMBO VYA HABARI
RPC
KATAVI ATANGAZA NAMBA YAKE YA SIMU KWA WANANCHI
*Yasaidia kumwokoa msichana aliyetaka
kubakwa
KAMANDA wa Polisi Mkoa wa Katavi, Kamishna Msaidizi wa
Polisi, Dhamiri Kidavashari ameamua kutangaza namba yake kwa wakazi wa wilaya
mpya ya Mlele, mkoani humo.
RPC Kidavashari ambaye anafuatana na Waziri Mkuu, Mizengo
Pinda kwenye ziara yake ya jimbo la Katavi, wilayani Mlele, ametumia fursa ya
utambulisho kwa wananchi kwa kutangaza namba yake ambayo ni 0769-168-850 ili
wananchi wampatie taarifa kuhusu matukio ya uhalifu.
Aliwaeleza wananchi katika kata na vijiji mbalimbali
ambavyo Waziri Mkuu amepitia kwamba ulinzi wa nchi na uwepo wa amani unategemea
ushiriki wa wananchi na kwamba suala hilo si la polisi peke yake. Aliwasihi
wawe wepesi kutoa taarifa pale wanapohisi kuna jambo ambalo si la kawaida.
Katika mahojiano maalum, jana jioni (Jumatatu, Desemba 18,
2012), Afande Kidavashari alisema uamuzi wake wa kutangaza namba ya simu ni
sehemu ya utekelezaji wa sera ya polisi jamii ambayo inatekelezwa Kitaifa.
“Sasa hivi hata ukiingia kwenye mabasi, utakuta namba za
Makamanda wa Polisi wa Mikoa zimebandikwa ndani ya mabasi ikiwa ni njia ya
kupunguza ukiritimba wa kupokea taarifa kutoka kwa wananchi... pia ni njia ya
kuturahisishia mawasiliano na kutuweka karibu na wananchi,” alisema.
Alipoulizwa kama hatua yake hiyo imeleta manufaa yoyote,
Afande Kidavashari alikiri kupokea taarifa zilizosaidia binti mmoja asibakwe na
vijana wa bodaboda mwishoni mwa wiki iliyopita. “Kuna raia mwema aliona vijana
wakimvamia binti mmoja katika eneo moja hapa Mpanda, akanipigia simu, nikatuma
askari ambao waliwahi katika eneo la tukio na kumwokoa yule msichana. Vijana
wawili walikamatwa na mmoja alikimbia, bado tunamfuatilia,” alisema.
Akitoa mfano mwingine, afande huyo alisema kuna meseji
(sms) aliipokea kutoka Ugalla mara baada ya Waziri Mkuu kufanya mkutano katika
kata hiyo ambapo kuna mkazi mmoja alionewa na watu wa Kaliua. “Mimi niliituma
ile sms kwa RPC Tabora naye akaituma kwa Kamanda wa Polisi Wilaya ya Kaliua
(OCD) na wameniarifu kuwa suala hilo tayari limeanza kushughulikiwa,”
aliongeza.
Akizungumzia aina ya matukio ya uhalifu yanayotokea mara
kwa mara mkoani humo, Kamanda huyo wa polisi alisema mengi ni ya uhamiaji
haramu, uvuvi haramu, wizi wa ng’ombe, wizi wa mbao kwenye misitu ya hifadhi na
uingizaji wa silaha haramu.
(mwisho)
IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU,
JUMANNE, DESEMBA 18, 2012.
No comments:
Post a Comment