TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
WAZIRI MKUU AKAGUA MRADI WA
UMWAGILIAJI UGALLA
WAZIRI MKUU Mizengo Pinda ametembelea
mradi wa umwagiliaji wa Ugalla na kusifu juhudi za wananchi wa kata hiyo katika
wilaya mpya ya Mlele mkoani Katavi.
Alikuwa akizungumza na wakazi wa
kijiji cha Ugalla kata ya Ugalla mara baada ya kukagua mradi huo
akiwa katika siku ya nne ya ziara yake jimboni kwake Katavi wilayani Mlele,
mkoani Katavi jana mchana (Jumapili, Desemba 16, 2012).
Alisema anawashukuru wakazi hao kwa
kuibua mradi huo ili waweze kunufaika na maji ya mto Ugalla ambao unapita
jirani. Pia aliwataka waheshimu uamuzi wao wa kutoa eneo hilo kwa mradi ili
kuepuka migogoro ya umilikaji wa kifamilia na kiukoo.
“Ninawasihi muelewane ili kuepuka
migogoro ya maeneo. Mkishaanza kuvuna wako watakaodai kuwa hapa nilipewa na
babu yangu, hapa nilipewa na babu wa babu, wataanza kudai fidia. Ni vema
mkaelewana mapena juu ya umiliki wa enepo la mradi,” alisema.
Akitoa maelezo kwa Waziri Mkuu ambaye
ni mbunge wa jimbo hilo, Mhandisi Mkazi wa Umwagiliaji Kanda
ya Mbeya, Bw. Elibariki Mwendo alisema wamejenga tanki la kuhifadhi maji lenye
ujazo wa lita 530,000 ambazo zinaweza kumwagilia hekta 225.
Alisema mitambo ya kupandisha maji
kwenye tanki hilo itaendeshwa kwa kutumia nguvu ya umeme wa jua pamoja na umeme
unaozalishwa kwa nguvu ya upepo.
Mradi huo ulioibuliwa na wananchi
mwaka 2007 kupitia zoezi la fursa na vikwazo vya maendeleo, umegharimu sh.
milioni 778. Unamilikiwa na wanachama 146 na utahudumia watu 3,077.
Kesho (Jumanne, Desemba 18, 2012)
Waziri Mkuu atakwenda kata ya Sitalike ambako atahutubia wananchi.
(mwisho)
IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU,
No comments:
Post a Comment