Na Thehabari.com
KAMPUNI
ya JR & LK Investment inatarajia kuzinduwa tuzo yake ya kwanza kwa
wasanii wa Muziki wa Asili itakayojulikana kama 'Mwalimu Nyerere
Tanzania Contemporary Traditional Muzic Awards'
Tuzo hiyo inatarajia kuwakumbuka wasanii wa nyimbo za asili ambazo
ndizo zinazobeba utamaduni wa Mtanzania, ambao umekuwa ukifunikwa na
tamaduni za nje kwa muda.
Akizungumza na waandishi wa habari leo
jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi wa JR & LK Investment, Mchatta Eric
Mchatta alisema kampuni hiyo tayari imepewa kibali na
Baraza la Sanaa Tanzania (BASATA) kuendesha tuzo hizo.
Alisema
kwa mara ya kwanza tuzo hizo zinatarajiwa kuanzishwa kwenye wiki ya
kumbukumbu ya kifo cha Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere itakayofanyika kuanzia Oktoba 11, 2013.
Aidha alisema tuzo hizo zina lengo la kuthamini na kuinua kazi za
wasanii wa asili, kubadilisha tamaduni na kuheshimu wanamuziki wa asili
Tanzania.
"Mwalimu Nyerere katika siku za uhai wake aliwahi
kusema; "Taifa bila tamaduni ni sawa na taifa lililo kufa, kwa
kuzingatia usemi huo wa Mwalimu Nyerere, JR & LK Investment
imedhamiria kwa dhati kuwainua wanamuziki wanao fanya muziki wa asili
kwa njia ya kuwashindanisha kwa kupigiwa kura na wananchi...," alisema
Mchatta.
Alisema kwa sasa Tanzania imepoteza baadhi ya tamaduni, mila, na
desturi zake na badala yake kufuata tamaduni za mabara mengine kama
Ulaya na sehemu nyinginezo. "Tuzo za muziki asili za Mwalimu Nyerere
zinalenga pia kuwaleta Watanzania wa kila rika, kabila, dini na
wanaofanya kazi anuai kuungana na kujifunza uzuri na thamani ya
kudumisha tamaduni...," alisema kiongozi huyo.
JR & LK Investment imewaomba Watanzania kukaa mkao wa kuunga
mkono tuzo hizo ikiwa ni pamoja na wadau kujitokeza kufanikisha shughuli
hiyo inayotarajia kuinua muziki wa asili nchini.
*Imeandaliwa na www.thehabari.com
No comments:
Post a Comment