TANGAZA NASI LEO 0712709630,0756631636 BARUA PEPE gmkojera@gmail.com

Wednesday 6 March 2013

Waangalizi wa kanda:Upigaji kuru Kenya ulikuwa ‘’dole tupu’’

Na  Isaac Mwangi, EANA
Arusha, Machi 6, 2013 (EANA) – Waangalizi wa Kanda katika uchaguzi mkuu wa Kenya wameonyesha kuukubali mwenendo wa upigaji kura Jumatatu kuwa ulikwenda sawia na kutaka hali hiyo iendelee katika hatua nyingine zilizobaki za uchaguzi huo.

Taarifa hiyo imetolewa na Timu ya Pamoja ya Waangalizi wa Kanda kutoka Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC), Soko la Pamoja la Nchi za Mashariki na Kusini mwa Afrika (COMESA) na Mamlaka ya Maendeleo Afrika (IGAD), Shirika Huru la Habari la Afrika Mashariki (EANA) limeripoti.

‘’Ingawa kulikuwepo na changamoto kadhaa kuhusu uhakiki wa wapiga kura, timu hiyo imehitimisha kwamba uchaguzi mkuu wa 2013 umefikia viwango vya kanda, bara na vya kimataifa kuwa ni wa kuaminika na uwazi,’’ ilieleza taarifa iliyotolewa Jumanne.

Taarifa ya awali ya waangalizi imetathmini hali ya kisiasa kuelekea kwenye uchaguzi,uteuzi wa wagombea uliofanywa na vyama vya siasa, kampeni na nafasi ya wapiga kura na vyombo vya habari kwenye mchakato mzima wa uchaguzi huo.

Timu hiyo katika taarifa yake imeleza pia kwamba ilitathmini siku ya upigaji kura yenyewe ikiwa ni pamoja na idadi ya watu waliojitokeza kupiga kura,mwenendo wa upigaji kura,wasimamizi,masuala ya usalama,waangalizi na mawakala wa vyama vya siasa.

Taarifa hiyo ya Timu, iliipongeza Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) kwa kusimamia uchaguzi huo kwa weledi, pia iliwapongeza maafisa usalama kwa kuhakikisha kwamba sheria na taratibu zinafuatwa katika kipindi chote cha mchakato wa upigaji kura.

‘’Matukio machache ya ghasia hayakuweza kufunika mwendendo mzima wa amani katika uchaguzi huo,’’ taarifa ilisisitiza.

Taarifa hiyo ya waangalizi pia iliguswa na idadi kubwa ya kura zilizoharibika ambazo zinaweza kuleta athari katika matokeo. Ilisema hiyo inawezekana imetokana na wapiga kura kutoelewa sawia taratibu za upigaji kura.

Taarifa hiyo ilisomwa na Kiongozi wa Timu ya Waangalizi wa Uchaguzi ya Kanda, Abdulrahman Kinana aliyefuatana na viongozi wenzake wa timu za waangalizi za COMESA, EAC na IGAD.

Kinana ambaye ni Spika wa zamani wa Bunge la Afrika Mashariki (EALA) alitoa wito kwa wagombea kuyakubali matokeo ya uchaguzi huo au kama wana malalamiko watumie njia inayokubalika ya kuyafikisha mahakamani.

Makundi hayo matatu ya kanda yalikuwa na jumla ya waangalizi 78 waliosambazwa katika kaunti 40 kati ya 47 zilizopo nchini Kenya.
IM/LC/NI

No comments:

Post a Comment