Mkurugenzi Mtendaji wa Mtandano wa Jinsia Tanzania(TGNP) Usu Mallya |
Akizungumza na Blogu hii, Mwenyekiti wa
Wanawake Katoliki Tanzania ( WAWATA) Bi. Olive Luena amesema wananawake wana changamoto ya
kuliombea taifa ambalo kwa sasa liko katika kipindi kigumu cha mahusiano kati
ya dini na dini na watu kujichukulia sheria mkononi.
Bi. Luena amesema wanawake wote bila kujali dini zao
wafunge na kuombea taifa amani ili iweze kuwepo kuanzia ngazi ya familia hadi
taifa.
“Wanawake tukae pamoja, tumlilie Mungu aliokoe taifa
letu lisiingie katika machafuko ambayo dalili zake zimeanza kuonekana na kuleta
hofu kwa watu wetu,” amesema.
Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Mtandao wa Jinsia Tanzania Usu
Mallya anaeleza kuwa ukosefu wa uelewa wa masuala ya kijinsia ni kikwazo
kikubwa cha kupambana na tatizo la ukatili wa kijinsia katika ngazi ya jamii
hadi kitaifa.
“Kuna changamoto kubwa ya kukosekana kwa uelewa
mpana wa dhana ya usawa na haki za kijinsia ambayo imesababisha hata mgawanyo
wa rasilimali katika maeneo mbalimbali kutozingatia hali halisi na mahitaji ya
kijinsia , mfano uandaaji wa bajeti za kiserikali, ujenzi wa miundombinu,
utoaji wa huduma za kijamii kama maji, afya na
chakula,”anasema.
Anasema kutokana na changamoto hizo wanatumia fursa
ya siku ya wanawake kupaza sauti zao kudai haki ya kuangalia suala la usawa wa
kijinsia, wanawake wanapata haki zao za msingi hasa katika suala la matibabu,
uzazi salama, elimu, maji salama, ushiriki wa kutosha katika nafasi za ajira
ngazi zote na ushiriki sawa katika nafasi za maamuzi na ulinzi wa kutosha
kutokana na kukithiri kwa ukatili wa kijinsia.
Mallya anasema “tumetambua kuwa uelewa wa masuala ya
kijinsia ni pamoja na kuyaingiza kwenye katiba mpya kama sheria mama ya nchi,
kuweka mikakati ya kuingiza masuala ya wanawake katika sera, mipango na bajeti
kila mwaka,”.
Naye Mkurugenzi wa Mfuko wa wanawake Tanzania (TWF)
Mary Rusimbi anabainisha kuwa uelewa wa masuala ya kijinsia kwa wanawake na wanaume umeongezeka , ingawa
bado wanaonekana kurudi nyuma na kuruhusu ukatili wa kijinsia kuendelea
kufanyika nchini kuanzia majumbani, sehemu za kazi na maeneo mengine.
Anasema jambo la kufanya, ni asasi mbalimbali nchini
ziungane na kuwa kitu kimoja katika
kuhakikisha kuwa zinaendelea kutoa elimu kuanzia vijijini ili kujenga uelewa
zaidi kwa jamii.
Anasema ni muhimu
wanawake wawe wahitaji na kuunganisha nguvu zao ili mabadiliko makubwa
yaweze kutokea. Wasipokuwa ni wahitaji
nani atawasemea?
Mama Rusimbi anasema siku za nyuma Wizara ndio
ilikuwa ina kazi kubwa ya kwenda kuelimisha jamii, lakini kwa sasa kuna asasi
nyingi ambazo zimekuwa mstari wa mbele
katika kutoa elimu, zinahitajika kutumia fursa walizonazo na kuongeza kasi ya
uelewa hasa katika maeneo ambayo bado
hayajapata elimu ya kutosha kuhusiana na masuala ya kijinsia.
Lakini anawakumbusha watunga sera na waandaji wa bajeti,
kuweka mkakati wa pamoja utakaolenga kuwaletea wanawake maendeleo.
Kwa upande wake, Katibu Mkuu Msaidizi wa Umoja wa
Mataifa na Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la
Umoja wa Mataifa la Idadi ya Watu (UNFPA) Dk. Babatunde Osotimehin anaeleza
kuwa duniani kote wanawake na wasichana wanakabiliwa na vitendo mbalimbali vya
ukatili wa kijinsia ikiwa ni pamoja na
ubakaji,ukeketaji, ndoa za utotoni na ukatili wa kingono.
“Tukiwa miongoni mwa jumuiya ya kimataifa tuna
jukumu la kuhakikisha ukiukwaji wa haki za binadamu unatokomezwa,”anasema.
Anasema hii ni changamoto kubwa ambayo inaweza
kufanyiwa kazi ikiwa tu wanawake wataungana na kuwa na lengo moja la
kuhakikisha kuwa wanawake na wasichana wanakuwa salama dhidi ya vitisho vya
ukatili wa kijinsia.
“Hii ni fursa yetu ya kuleta mabadiliko chanya kwa
maisha ya mamilioni, hatuwezi kupoteza fursa hii,”anasema.
Aidha, Afisa tawala na Mratibu wa Masuala ya Jinsia
na Ukimwi wa Wizara ya Katiba na Sheria Joyce Mloe anasema bado kuna changamoto
kubwa kuhusiana na uelewa wa masuala ya
kijinsia kwa jamii, watu wanafikiri yanahusu wanawake pekee kumbe ni jambo la
watu wote.
“Kuna umuhimu mkubwa wa kutolewa kwa elimu ya
kutosha kuhusiana na masuala ya jinsia, na sisi kama Wizara ya Katiba na Sheria
tunaendelea na mkakati wetu wa kuelimisha jamii, kuhusu sheria mbalimbali na
masuala ya jinsia kupitia vyombo vya habari,”anasema.
Anasema Wizara imeanzisha dawati maalum ambalo huwa
linatoa huduma za kisheria kwa wananchi wenye matatizo mbalimbali
Mloe anasema
wanawake waungane kusimamia haki zao hasa kwa kujitokeza katika mchakato wa
ukusanyaji wa katiba mpya na kuzungumzia sheria zote kandamizi ili hatimaye
ziweze kurekebishwa.
Hata hivyo, bado makundi yaliyoko pembezoni
hayatanufaika ipasavyo huduma zilitolewazo na Wizara hiyo kwa vile huduma zao
nyingi zipo mjini. Nilipohoji vipi kuhusu walioko pembezoni watahudumiwaji
ikiwa wengine hawana redio na runinga.
Kwa mujibu wa Mloe anasema kuwa elimu ya sheria na
huduma za sheria na haki za binadamu zitafika maeneo ya vijijini kwa kutegemea
zaidi kutoa elimu yao kupitia vyombo vya habari.
Hata hivyo, Siku ya wanawake duniani imekuwa ikitumiwa na wanawake kukaa kwa pamoja na kujadili
changamoto ambazo zimekuwa zikiwakabili
wanawake ikiwa na lengo ya kuzitafutia ufumbuzi ili hatimaye waweze
kupata haki zao.
Maadhimisho ya mwaka huu yanaoongozwa na kauli mbiu
inayosema “Uelewa wa masuala ya jinsia
katika jamii:Ongeza kasi”.
Uelewa wa masuala ya jinsia katika jamii huelezwa
bado ni kikwazo kikubwa katika maendeleo ya wanawake Tanzania kutokana na mfumo
uliojenga tangu enzi za mababu. Ni asilimia ndogo ya watu wanauelewa wa kutosha
kuhusiana na masuala hayo lakini asilimia kubwa ya makundi yaliyokuwa pembezoni
hayaelewi kutokana na mfumo unaoelezwa kuwa ni Ubepari.
Ili uelewa uweze kufika, wanawake wote walioko
katika makundi yao ni kutumia fursa walizonazo kuelimisha wengine. Inawezekana
ikiwa wanawake watakuwa na umoja.
No comments:
Post a Comment