Rais wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete ameyaalika na kuyakaribisha makundi
mbali mbali katika jamii kupendekeza majina ya watu ambao Rais atayafikiria
katika uteuzi wa Wajumbe wa Bunge Maalum la Katiba.
Rais Kikwete ametoa mwaliko huo
kulingana na mamlaka anayopewa katika Kifungu cha 22(1) (c) cha Sheria ya
Mabadiliko ya Katiba (Sura ya 83) na aliutangaza rasmi mwaliko huo katika
Gazeti la Serikali Na. 443 la Ijumaa iliyopita, Desemba 13, 2013.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa Dar
es Salaam leo, Ijumaa, Desemba 20, 2013 na Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Ombeni
Sefue, mwaliko huo ambao pia utatangazwa katika magazeti ya kawaida, makundi
yaliyokaribishwa kutoa mapendekezo yametakiwa kuwasilisha kwa Rais orodha ya
watu wasiopungua wanne na wasiozidi tisa kwa kila kundi.
Makundi hayo ambayo yametajwa katika
Sheria ya Mabadiliko ya Katiba ni Taasisi zisizokuwa za Kiserikali, Taasisi za
kidini, Vyama vyote vya siasa vyenye usajili wa kudumu, Taasisi za elimu ya
juu, Makundi ya watu wenye ulemavu, Vyama vya wafanyakazi, Vyama
vinavyowakilisha wafugaji, Vyama vinavyowakilisha wavuvi, Vyama vya wakulima na
Makundi mengine yenye malengo yanayofanana.
Taarifa ya Balozi Sefue inasema kuwa
katika kuwasilisha mapendekezo ya majina yao, makundi yaliyoalikwa yanalazimika
kuonyesha umri, jinsia, uzoefu, sifa na sehemu ya makazi ya mtu anayependekezwa
ikiwa ni pamoja na kuzingatia usawa wa kijinsia.
Katika mwaliko wake, Rais Kikwete
ameelekeza kuwa orodha ya majina ya wanaopendekezwa, iwasilishwe kwa maandishi
ama kwa kupelekwa na mtu kwa mkono ama kwa kutumia huduma ya Posta.
Orodha hizo ziwasilishwe kupitia
anuani zifuatazo:
1.
Katibu Mkuu Kiongozi
Ofisi ya Rais, Ikulu,
S.L.P. 9120,
Dar
Es Salaam
ama
2.
Katibu Mkuu Kiongozi,
Ofisi ya Rais,
S.L.P. 4224,
Zanzibar
Taarifa ya Balozi Sefue inasema kuwa
tarahe ya mwisho ya kupokea orodha ya majina yanayopendekezwa ni Januari 2,
2014.
“Mwisho”
No comments:
Post a Comment