TANGAZA NASI LEO 0712709630,0756631636 BARUA PEPE gmkojera@gmail.com

Thursday 12 December 2013

Pinda: Niondoeni




WAZIRI Mkuu, Mizengo Pinda, amesema atafurahi akiondolewa madarakani kwa kuwa kazi anayoifanya ni sawa na kubeba Msalaba mzito. 
Pinda aliongeza kuwa iwapo anaonekana mzigo, Rais Jakaya Kikwete anaweza kutengua uteuzi wake na akishindwa wabunge wana fursa ya kupiga kura ya kutokuwa na imani naye.


Kauli hiyo aliitoa jana bungeni alipokuwa akijibu swali la papo kwa papo, aliloulizwa na mbunge wa viti maalum, Rukia Kasim Mohamed (CUF), aliyetaka kujua msimamo wake baada ya kutajwa ni mzigo namba moja katika serikali.

“Tulipokuwa tukijadili taarifa za kamati mbalimbali mbunge mmoja wa CCM alinukuu kauli ya Katibu Mkuu wa CCM kuwa wapo mawaziri mizigo….mbunge huyo alisema wewe Waziri Mkuu ni mzigo namba moja, je unaisemaje kauli hii?” alihoji.

Akijibu swali hilo, Pinda alisema anasimamia zaidi ya wizara 20 hivyo kumuita mzigo kwa sababu ya kutofanya vizuri kwa wizara moja au mbili ni kutomtendea haki.

“Huwezi kuwa mzuri katika kila sehemu, inawezekana mbunge alikuwa na mawazo yake lakini angeweza kuniambia mimi sikupendi kwa sababu ya moja mbili tatu hapo mimi nafikiri ningeweza kujua nifanye nini,” alisema.

Pinda alisema anaweza kuondoka madarakani iwapo Rais Kikwete, ataamua kutengua uteuzi wake lakini akishindwa wabunge wana fursa ya kufanya hivyo kwa kupiga kura ya kutokuwa na imani na Waziri Mkuu.

Aliongeza kuwa kama ikitokea Bunge likapiga kura hiyo yuko tayari kuwekwa kiti moto (kujieleza) na kama ikibidi ataondoka madarakani kwa kuwa kazi hiyo ni kujitwisha Msalaba.

“Dada Rukia kama utafikia mahali unaona mimi sifai na ukaungana na wabunge wote kuniondoa ……nitafurahi kwelikweli maana angalau nitapumua kidogo kazi hii ni nzito sana; tunaibeba kama msalaba,” alisema.

Pinda aliongeza kuwa yeye na mawaziri wenzake wamekuwa wakifanya jitihada kubwa kuyatimiza majukumu waliyonayo lakini kwa kuwa binadamu si wakamilifu makosa hujitokeza.

Alisema uwaziri mkuu usiwasumbue wabunge kwa sababu kazi hiyo haiombwi bali ni uteuzi wa Rais anayeona nani anafaa kuishika na akiona mhusika haifanyi vizuri humuondoa.

Wiki iliyopita mbunge wa Mwibara, Kangi Lugola (CCM), alisema mchawi wa maendeleo ya nchi ni Waziri Mkuu Pinda na pia ni mzigo namba moja kwa sababu amezidisha upole katika kuwasimamia mawaziri na watumishi wanaofanya ufisadi.

Lugola alimtaka Pinda na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Hawa Ghasia, wajiuzulu mara moja.

Shutuma za baadhi ya mawaziri kuwa mizigo zimekuwa zikitolewa mara kwa mara ambapo hivi karibuni Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana, Katibu wa Itikadi na Unezi, Nape Nnauye, walisema Kamati Kuu (CC) ya chama hicho itawahoji mawaziri hao.

Viongozi hao wa CCM wakiwa katika mikoa ya Mtwara, Mbeya, Njombe na Ruvuma walisema baadhi ya mawaziri hawawajibiki ipasavyo hali inayowafanya wananchi waichukie serikali.
Migiro aapishwa

Aliyekuwa Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Asha-Rose Migiro, jana alikula kiapo cha utii baada ya kuteuliwa na Rais Jakaya Kikwete kuwa mbunge.

Migiro alipokelewa na kina mama wa CCM huku baadhi ya wabunge wakipiga vigelegele pamoja na makofi na baadaye alisema kazi ya ubunge ni utumishi kama ulivyo utumishi mwingine hivyo ni wajibu wa kila mbunge kuwatendea haki wananchi.

“Mbunge ni sawa kama mtumishi mwingine, haijalishi ni mbunge wa jimbo au wa kuteuliwa, cha msingi ni kufanya kazi na kila mtu bila kujali itikadi ya chama chako,” alisema.

Chanzo Tanzania Daima

No comments:

Post a Comment