Polisi walilazimika kutumia gesi ya kutoa machozi kuwatawanya wafuasi wa Lukwago(Picha na Bbc swahili) |
Na Bbc Swahili
Meya wa mji mkuu wa Uganda, Kampala, ameondolewa
ofisini na madiwani baada ya jopo maalum kumpata na hatia ya matumizi
mabaya ya mamlaka yake pamoja na kutokuwa na ujuzi wa kutosha kwa kazi
yake.
Wafuasi wake wanaamini kuwa serikali ilipanga kumwondoa ofisini ili kuchukua wadhifa wa meya kutoka kwa upinzani.
Lukwago ni mwanachama wa chama cha upinzani cha Democratic Party (DP).
Alichaguliwa kama meya mwezi Januari mwaka 2011.
Wiki mbili zilizopita, serikali iliteua jopo lililomchunguza Lukwago na kuamua kuwa miongoni mwa makosa aliyoyafanya ni kukosa kuandaa mikutano muhimu , kupuuza wakuu waku wake na kuchochea umma kutolipa kodi.
Bwana Lukwago alitaja jopo hilo lililoongozwa na jaji kama, mahakama ya kipuuzi na kusema kuwa Rais Yoweri Museveni, ndiye aliyechochea jambo la kumwondoa ofisini ili washirika wake waweze kuchukua madaraka, baada ya kushindwa kwenye uchaguzi wa mwaka 2011.
Vurugu zilizuka na kutatiza usafiri mjini Kampala baada ya wafuasi wa Bwana Lukwago kupinga kuondolewa kwake ofisini.
No comments:
Post a Comment